Viongozi wa Hizbullah, Jihad Islami wakutana kujadili matukio ya Palestina
Katibu Mkuu wa Harakati ya Hizbullah ya Lebanon Sayyed Hassan Nasrallah amekutana na kiongozi wa harakati ya Jihad Islami ya Palestina.
Ofisi ya uhusiano wa umma ya Hezbullah ilitangaza Jumapili kwamba Nasrallah alimpokea Ziad al-Nakhaleh katika mji mkuu Beirut, na viongozi hao wawili walibadilishana mawazo juu ya matukio ya hivi karibuni huko Palestina, Lebanon na eneo zima la Asia Magharibi.
Mohammed al-Hindi, mkuu wa ofisi ya kisiasa ya Jihad Islami pia aliandamana na Nakhaleh katika mkutano huo na mkuu wa Hezbullah.
Ofisi ya uhusiano wa umma ya Hezbullah imesema katika taarifa kwamba: "Tathmini ya matukio ilifanyika wakati wa mkutano huo, ambapo changamoto na fursa za Mhimili wa Muqawama (Mapambano ya Kiisalmu) pia zilijadiliwa."
Mapema mwezi huu, Nasrallah alikutana na Ismail Haniyeh, mkuu wa ofisi ya kisiasa ya Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina, Hamas. Pande hizo mbili pia zilibadilishana mawazo kuhusu kanda na changamoto zinazokabili harakati za Muqawama.
Katika kipindi cha miezi kadhaa iliyopita, utawala haramu wa Israel umeongeza mashambulizi katika miji na maeneo mbali mbali ya Palestina. Kutokana na mashambulizi hayo makumi ya Wapalestina wameuawa shahidi na wengine wengi kukamatwa.
Zaidi ya Wapalestina 200 wameuawa shahidi na Israel tangu mwanzoni mwa mwaka huu, wakiwemo watoto 36.
Umoja wa Mataifa umeonya kuwa mwaka 2023 unakaribia kuwa mwaka mbaya zaidi kwa Wapalestina tangu uanze kurekodi vifo.
Takriban Wazayuni 26 wameangamizwa katika mashambulizi ya ulipizaji kisasi ya Wapalestina.