Hizbullah: Lebanon haina haja na nasaha na ushauri wa Wamarekani
-
Sayyid Hashim Safiuddin
Mkuu wa Baraza la Utendaji la Hizbullah ya Lebanon amejibu matamshi ya hivi karibuni ya mwakilishi wa Marekani mjini Beirut na kusisitiza kuwa, Lebanon haina haja ya nasaha na ushauri wa Wamarekani.
Katika hatua yake ya kuingilia waziwazi mambo ya ndani ya Lebanon, Amos Hochstein, mjumbe wa Marekani mjini Beirut amesema kuwa, wakati umefika wa kuchorwa mipaka ya ardhini ya Lebanon na utawala wa Kizayuni wa Israel, ikiwa ni sehemu ya hatua zinazochukuliwa na Marekani za kufuatilia makubaliano ya baharini kati ya Lebanon na utawala wa Kizayuni.
Kwa mujibu wa shirika la habari la IRNA, Hashim Safiuddin, Mkuu wa Baraza la Utendaji la Hizbullahi ya Lebanon amesema, nchi yake haina haja na ushauri wa Marekani na mtu kama Hochstein ambao wameiwekea vikwazo Lebanon isiweze kupokea misaada ya kiuchumi.
Hashem Safieddin ameongeza kuwa, kama kweli Marekani ina nia njema, basi itekeleze tu ahadi zake ndogo kwa Walebanon kuhusu suala la kuiruhusu nchi hiyo kuingiza gesi kutoka Misri.
Mkuu wa Baraza la Uutendaji la Hizbullah ya Lebanon amesisitiza kwamba nchi yake haitokuwa karibu na Marekani kwani Marekani ni adui wa wazi wa wananchi wa Lebanon. Wananchi wa Lebanon hawezi kusahau jinai ya mauaji ya "Qana" na mauaji mengine yote yanayofanywa kwa silaha za Marekani ndani ya Lebanon, huko Palestina na katika maeneo mengine ya Waislamu.
Amesema, Wamarekani ndio chanzo kikuu cha matatizo ya hivi leo nchini Syria hususan kwa kutilia maanani wizi wa mafuta ya nchi hiyo na vizingiti vyake chungu nzima vya kuzuia uwekezaji unaofanywa na nchi za Kiarabu huko Syria.
Mkuu wa Baraza la Utendaji la Hizbullah ya Lebanon ameongeza kuwa, muqawama ulioikomboa ardhi ya Lebanon utayakomboa pia maeneo mengine ya ardhi inayokaliwa kwa mabavu ya nchi hiyo na daima muqawama utakuwa tayari kuilinda Lebanon dhidi ya adui Mzayuni kwa tishio lolote lile.