Hamas yakanusha madai ya Israel kuhusu kuendesha " kamandi ya kivita" hospitalini
Harakati ya Kiislamu ya Kupigania Ukombozi wa Palestina, Hamas, imekanusha madai ya utawala wa Kizayuni wa Israel kuwa eti ina 'kamandi ya kivita' iliyo katika eneo la chini ya hospitali kubwa zaidi ya Ukanda wa Gaza, ambayo imekuwa ikikabiliwa na hujuma ya kijeshi ya utawlaa huo.
Osama Hamdan, mwakilishi mkuu wa harakati hiyo nchini Lebanon, alikanusha madai ya Israel kwa kuwasilisha ushahidi wa picha wakati akizungumza mjini Beirut siku ya Alhamisi.
Kanda hiyo ilionyesha kuwa utawala huo umeingiza kwa siri silaha katika Hospitali ya al-Shifa, kabla ya kudai kuwa ilizipata ndani ya kituo hicho cha afya.
Klipu hiyo imeonyesha namna vikosi vya utawala haramu wa Israel vimekuwa vikikusanya silaha katika maeneo mbali mbali ya Gaza na kuzipeleka hadi kwenye hospitali hiyo ndani ya masanduku yenye lebo ya chakula cha msaada.
Israel ilianzisha vita dhidi ya Gaza tarehe 7 Oktoba baada Hamas kuendesha operesheni ya Kimbunga cha al-Aqsa dhidi ya Isreal ikiwa ni katika kukabiliana na jinai za Israel za miongo kadhaa za umwagaji damu na uharibifu dhidi ya Wapalestina.
Kwa mujibu wa wizara ya afya ya Gaza, Israel imewaua Wapalestina wasiopungua 11,500, wakiwemo watoto 4,630 na wanawake 3,130, na kujeruhi wengine zaidi ya 32,000.
Hospitali zimekuwa kitovu cha mashambulio makali ya utawala dhalimu wa Israel tangu kuanza vita.
Siku ya Jumatano, mkuu wa Idara ya Mifupa huko al-Shifa alisema buldoza na vifaru vya Israel vilivamia kituo hicho, na kubomoa sehemu za majengo hayo.
Mashambulizi dhidi ya hospitali ni kinyume cha sheria za kimataifa na Mikataba ya Geneva inayotaja vituo vya matibabu kama miundombinu ya kiraia.
Hamas imeutaka Umoja wa Mataifa kuunda timu ya uchunguzi ili kufichua madai ya Tel Aviv kuhusu hospitali hiyo.