Wakati anatumikia kifungo jela, Imran Khan ateuliwa kuwania Tuzo ya Amani ya Nobel
(last modified Wed, 02 Apr 2025 10:31:28 GMT )
Apr 02, 2025 10:31 UTC
  • Wakati anatumikia kifungo jela, Imran Khan ateuliwa kuwania Tuzo ya Amani ya Nobel

Waziri Mkuu wa zamani wa Pakistani Imran Khan aliyefungwa jela, ameteuliwa kuwania Tuzo ya Amani ya Nobel kwa "kazi aliyofanya kuhusiana na haki za binadamu na demokrasia nchini Pakistan". Hayo yameelezwa katika tamko lililotolewa na chama cha siasa cha Norway Partiet Sentrum.

Uteuzi huo umefanywa kwa ushirikiano na wanachama wa Muungano wa Pakistan World Alliance (PWA), kundi la kutetea haki lililoundwa mwezi Desemba 2024.
"Tunafuraha kutangaza kwa niaba ya Partiet Sentrum kwamba, kwa ushirikiano na mtu aliye na haki ya kuteua, tumemteua Imran Khan, waziri mkuu wa zamani wa Pakistan, kwa ajili ya Tuzo ya Amani ya Nobel," imeeleza taarifa ya chama hicho kupitia ujumbe uliowekwa kwenye mtandao wa X.
 
Hii ni mara ya pili kwa Khan mwenye umri wa miaka 72 kuteuliwa kuwania tuzo hiyo. Mnamo mwaka 2019, waziri mkuu huyo wa zamani wa Pakistan alitambulika kwa juhudi zake za kuimarisha amani katika eneo la Asia Kusini.
 
Kamati ya Nobel ya Norway hupokea mamia ya teuzi kila mwaka na kuchagua mshindi kupitia mchakato mkali wa uchujaji unaochukua muda wa miezi minane.

Khan, ambaye ni mwanzilishi wa chama cha upinzani cha Pakistan Tehreek-e-Insaf (PTI), amefungwa jela tangu Agosti 2023. Mnamo mwezi Januari, alihukumiwa kifungo cha miaka 14 katika kesi ya 'ufisadi' kwa kinachodaiwa kuwa ni matumizi mabaya ya mamlaka, ikiwa ni hukumu ya nne dhidi yake.

Kesi alizohukumiwa kabla, ya zawadi za serikali, uvujishaji wa taarifa za siri, na ndoa isiyo halali zilikuja kubatilishwa au kusimamishwa baadaye.

Nyota huyo wa zamani wa kriketi aliyegeuka kuwa mwanasiasa aliondolewa madarakani Aprili 2022 baada ya kupigiwa kura ya kutokuwa na imani naye na Bunge. Hata hivyo Khan amekana mashtaka yote dhidi yake akisisitiza kuwa yamechochewa na sababu za kisiasa.../