Ripoti: Mossad yaahirisha mpango wa hujuma ya nchi kavu dhidi ya Hamas Nchini Qatar
IQNA – Shirika la ujasusi la Israel, Mossad, limeahirisha mpango wa uvamizi wa nchi kavu uliolenga kuwaua viongozi wa Hamas walioko Qatar, mpango uliokuwa ukifanyiwa kazi katika wiki za hivi karibuni.
Hayo yamefichuka baada ya utawala wa Israel kufanya shambulizi dhidi ya eneo la makazi katika mji mkuu wa Qatar, Doha, mnamo Jumanne, likilenga viongozi wa Hamas waliokuwa wakikutana kujadili pendekezo la kusitisha mapigano huko Gaza.
Shambulizi hilo halikufanikiwa. Viongozi wa juu wa Hamas walinusurika, lakini wanachama watano wa kundi hilo kutoka Gaza pamoja na afisa mmoja wa usalama wa Qatar waliuawa shahidi.
Gazeti la The Washington Post, likinukuu Waisraeli wawili ambao hawakutajwa majina, liliripoti Ijumaa kuwa Mkurugenzi wa Mossad, David Barnea, alipinga mpango wa kuwaua viongozi wa Hamas walioko Qatar, akihofia kuwa hatua hiyo ingeathiri mahusiano ya kidiplomasia ambayo yeye na shirika lake wamejenga na serikali ya Qatar.
Qatar imekuwa mwenyeji wa viongozi wa Hamas na mpatanishi muhimu katika mazungumzo ya kusitisha mapigano kati ya Hamas na utawala wa Israel.
Mnamo Januari, Barnea alisisitiza kuwa Mossad itaendelea kuwalenga wale waliopanga operesheni ya Oktoba 2023 inayoongozwa na Hamas.
Ingawa maafisa wengi wa Israel wanakubaliana kuwa viongozi wote wa Hamas, hata walioko nje ya Gaza, wanapaswa kuuawa hatimaye, baadhi yao—akiwemo Barnea na Mkuu wa Majeshi Eyal Zamir—walitilia shaka muda wa kutekeleza shambulizi hilo.
Wakati huo, viongozi wa Hamas walikuwa wakikutana nchini Qatar kujadili pendekezo la kusitisha mapigano lililoletwa na Israel na Marekani, likilenga kuwaachilia mateka 48 wa Kiyahudi waliobaki.
Meja Jenerali Nitzan Alon, afisa mwandamizi wa jeshi la Israel anayehusika na mazungumzo ya mateka, hakushirikishwa katika kikao cha Jumatatu kilichojadili shambulizi hilo dhidi ya Doha. Viongozi wa Israel walidhani kuwa angepinga shambulizi ambalo lingeweza kuhatarisha maisha ya mateka.
Mgawanyiko huu wa ndani uliathiri namna shambulizi lilivyopangwa na nafasi ya mafanikio yake, na kuonyesha mgongano mpana wa maslahi ndani ya taasisi za usalama za Israel.
Hata hivyo, shambulizi la Jumanne la angani halikufanikisha lengo kuu la kuwaua viongozi wa juu wa Hamas. Badala yake, Hamas iliripoti kuwa maafisa wake watano pamoja na afisa mmoja wa usalama wa Qatar waliuawa. Chanzo kimoja kilicho karibu na tukio hilo kilisema, “Israel haikuwapata waliowalenga.”
Wachambuzi wameeleza kuwa kundi la maafisa wa Israel wanaomuunga mkono Netanyahu, akiwemo Waziri wa Mambo ya Kimkakati Ron Dermer na Waziri wa Ulinzi Israel Katz, limechoshwa na mchakato wa mazungumzo.