Wapalestina wakumbuka ukatili wa Israel katika 'Mauaji ya Sabra na Shatila'
Leo Ijumaa tarehe 16 Septemba ni kumbukumbu ya ukatili wa kinyama uliotekelezwa na utawala wa Kizayuni wa Israel katika kambi za Wapalestina za Sabra na Shatila mjini Beirut Lebanon.
Katika tukio hilo la Septemba 16 mwaka 1982, wanajeshi wa utawala wa Kizayuni wa Israel wakishirikiana na wanamgambo wa kundi la Falanga wa Lebanon, walishambulia kambi za Wakimbizi wa Kipalestina za Sabra na Shatila mjini Beirut na kuwaua shahidi Wapalestina zaidi ya 3500.
Mauaji hayo ya umati yalitekelezwa kwa amri ya Ariel Sharon ambaye wakati huo alikuwa Mkuu wa Vikosi vya Kijeshi vya Israel. Mauaji hayo yalinyamaziwa kimya na vyombo vya habari; na hata madola yanayodai kutetea haki za binadamu ikiwemo Marekani na nchi za Magharibi zilinyamazia kimya jinai hiyo.
Tangu kuasisiwa utawala haramu wa Israel ulio dhidi ya binaadamu walimwengu wamekuwa wakishuhudia jinai za kuogofya za utawala huo ghasibu dhidi ya Wapalestina wasio na hatia. Mbali na jinai za Wazayuni huko Sabra na Shatila pia wametekeleza mauaji ya umati katika maeneo kadhaa ya Palestina kama vile Dier Yassin, Jenin na Ukanda wa Ghaza.