Makumi ya magaidi wa Daesh waangamizwa Deir ez Zor Syria
Wizara ya Ulinzi ya Russia imetangaza kuwa makumi ya magaidi ya kundi la Daesh wameuawa katika shambulio la ndege za kivita za nchi hiyo katika eneo la Deir ez Zor mashariki mwa Syria.
Wizara ya Ulinzi ya Russia imetangaza leo kuwa Gulmorad Halimov raia wa Tajikistan ambaye pia ni Waziri wa Vita wa kundi la kigaidi la Daesh (ISIS) na magaidi wenzake 44 wameuawa katika shambulio lililofanywa kwenye makao ya kundi hilo katika eneo la Deir ez Zor.
Taarifa ya Wizara ya Ulinzi ya Russia imeongeza kuwa, ndege za nchi hiyo zimezishambulia pia ngome kadhaa za kundi la Daesh huko Deir ez Zor.
Kwa mujibu wa data zilizothibitishwa, Abu Muhammad al Shamali raia wa Saudi Arabia ambaye anasimamia masuala ya fedha ya kuwaajiri magaidi na kuwasafirisha katika kambi za mafunzo za kundi la Daesh ni miongoni mwa vinara wa Daesh aliyeuawa huko Deir ez Zor.
Syria ilianza kukabiliwa na mgogoro mwaka 2011 kufuatia hujuma kubwa za makundi ya kigaidi yanayoungwa mkono na Saudi Arabia, Marekani na waitifaki wao ikiwemo Uturuki ili kuipindua serikali halali ya Rais Bashar Assad wa Syria.