Lavrov: Marekani inapasa kuondoka huko Syria
Waziri wa Mambo ya Nje wa Russia jana alisisitiza kuwa wanajeshi wa Marekani wanapasa kuondoka huko Syria haraka iwezekanavyo baada ya kupata pigo magaidi nchini humo.
Marekani imetuma wanajeshi wake huko Syria kinyume cha sheria bila ya idhini ya serikali ya Damascus kwa kisingizio cha kupambana na makundi ya kigaidi. Hii ni katika hali ambayo kama alivyokiri Rais Donald Trump wa Marekani; Washington ni chanzo kikuu cha kuibuka makundi ya kigaidi likiwemo kundi la ukufurishaji la Daesh. Ripoti rasmi zinaeleza kuwa, hadi kufikia sasa Marekani imewapatia magaidi walioko Syria na Iraq silaha za mabilioni ya dola na zana za kijeshi.
Viongozi wa Syria, wa nchi nyingine na taasisi za kimataifa wamesisitiza mara kadhaa kwamba hatua zinazotekelezwa na Marekani huko Syria ni sawa na ukaliaji mabavu. Shirika la habari la Farsi limeripoti kuwa, Sergei Lavrov ameeleza kuwa matamshi yaliyotolewa na viongozi wa Wizara ya Ulinzi ya Marekani (Pentagon) kwamba wanajeshi wa Marekani wana mpango wa kusalia huko Syria hadi itakapopatikana njia ya ufumbuzi wa kisiasa ya mgogoro wa nchi hiyo yameishangaza Russia.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Russia ameongeza kubainisha kuwa, viongozi wa Marekani hawawezi kuainisha njia ya ufumbuzi wa kisiasa huko Syria.
Syria ilitumbukia katika mgogoro mwaka 2011 kufutia hujuma kubwa iliyoanzishwa dhidi ya nchi hiyo na makundi ya kigaidi chini ya uungaji mkono wa Saudi Arabia, Marekani na waitifaki wao wa Magharibi na Kiarabu ili kubadili mlingano katika eneo la Mashariki ya Kati kwa maslahi ya utawala wa Kizayuni.