Utawala wa Kizayuni wakiri kuwauwa kwa umati Wapalestina
Polisi ya utawala wa Kizayuni imetangaza kuwa Wapalestina 201 ambao kuanzia mwezi Oktoba mwaka 2015 walishiriki katika oparesheni dhidi ya utawala huo wameuliwa hadharani.
Wananchi wa Palestina walianzisha Intifadha ya kuitetea Quds Tukufu tangu tarehe Mosi Oktoba mwaka 2015 kufuatia kushtadi jinai za utawala wa Kizayuni huko Quds na katika msikiti wa al Aqsa. Kanali ya habari ya Russia al Yaum leo asubuhi imeinukuu polisi ya utawala wa Kizayuni na kuripoti kuwa Wapalestina wanaotekeleza oparesheni za kufa shahidi wameuawa kwa kupigwa risasi moja kwa moja na wanajeshi wa Israel au polisi wa utawala huo bila ya kuhukumiwa.
Bunge la utawala wa Kizayuni (Knesset) tarehe tatu Januari mwaka huu lilipasisha sheria ya kuwanyonga Wapalestina ambao wanatekeleza oparesheni za kufa shahidi kwa kura za ndio 52 mkabala na 42 za hapana. Saleh al Aruri Naibu Mkuu wa Ofisi ya Kisiasa ya Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (Hamas) ameeleza kuwa kupasishwa sheria hiyo ya kunyongwa Wapalestina katika bunge la Knesset haina hatari ndogo kuliko uamuzi uliochukuliwa na Rais Donald Trump wa Marekani kuhusu Quds.
Rais wa Marekani tarehe sita mwezi Disemba mwaka jana aliutangaza mji wa Quds kuwa mji mkuu wa utawala wa Kizayuni; hatua iliyokabiliwa na upinzani na radiamali kubwa kutoka kwa wananchi, viongozi wa nchi na taasisi mbalimbali za kimataifa.