Wapalestina 2 wauawa shahidi kwa kombora la Israel, Gaza
Katika kile kinachoonekana ni mwendelezo wa ukatili na jinai, jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel limefyatua kombora kuelekea katika uzio wa Gaza na kuua shahidi Wapalestina wawili na kujeruhi wengine kadhaa.
Mauaji hayo ya kinyama yamefanyika siku mbili baada ya kijana mwingine wa Kipalestina kupigwa risasi na kuuawa na wanajeshi wa Israel kwa madai ya kuwajeruhi Wazayuni wawili karibu na mpaka wa Ukanda wa Gaza.
Utambulisho na majina ya Wapalestina waliouawa shahidi katika shambulizi hilo la kombora la Israel la usiku wa kuamkia leo katika kitongoji cha Qarara hayajajulikana.
Msemaji wa jeshi katili la utawala haramu wa Israel amedai kwamba, wanajeshi wa Kizayuni waliamua kuvurumisha kombora karibu na uzio wa Gaza, baada ya kuona kundi la vijana wa Kipalestina wakifukia ardhini 'kitu kisichojulikana'.
Maandamano ya haki ya kurejea makwao wakimbizi wa Palestina yalianza tarehe 30 Machi mwaka huu na yamekuwa yakiendelea kila Ijumaa katika mpaka wa Ukanda wa Gaza na maeneo mengine ya Palestina yanayokaliwa kwa mabavu na Wazayuni.
Ripoti ya Wizara ya Afya ya Palestina inaonesha kuwa, hadi hivi sasa zaidi ya Wapalestina 180 wameshauliwa shahidi na wanajeshi katili wa Israel na zaidi ya 19 elfu wengine wameshajeruhiwa.