Kuhani mmoja Myahudi-Mzayuni akutana na mfalme wa Saudi Arabia
Wizara ya Mambo ya Nje ya utawala wa Kizayuni wa Israel imetangaza kuwa, kuhani mmoja Mzayuni ameonana na mfalme wa Saudi Arabia mjini Riyadh.
Wizara ya Mambo ya Nje ya utawala wa Kizayuni ilitangaza habari hiyo jana na kuongeza kuwa, mfalme wa Saudia, Salman bin Abdulaziz amewakaribisha katika kasri yake ya Riyadh, wajumbe kutoka maeneo tofauti duniani akiwemo kuhani Mzayuni anayejulikana kwa jina la David Rosen.
Kabla ya hapo pia, Arthur Stark, mkuu wa lobi kubwa ya Kizayuni ya nchini Marekani AIPAC aliongoza kundi la wakuu wa ngazi za juu wa lobi hiyo kutembelea Saudi Arabia na kuonana na viongozi wa ngazi za juu wa nchi hiyo.
Baadhi ya nchi za Kiarabu zinazopakana na Ghuba ya Uajemi zikiwemo Saudi Arabia, Umoja wa Falme za Kiarabu (Imarati) na Bahrain huko nyuma zilikuwa na uhusiano wa siri wa miaka mingi na utawala wa Kizayuni wa Israel lakini hivi sasa zimeamua kuutangaza waziwazi uhusiano huo na zinapigana vikumbo katika kujaribu kuwa na uhusiano wa kirafiki na Israel ambayo mikono yake imejaa damu za wananchi wasio na hatia wa Palestina.
Nchi hizo za Kiarabu zinajitahidi kuwa na uhusiano wa kawaida na utawala wa Kizayuni wa Israel katika hali ambayo utawala huo pandikizi unafanya ukatili mkubwa dhidi ya Waislamu na wananchi wa kawaida hususan huko Palestina na katika maeneo mengi ya Kiarabu na Kiislamu.