Saudia kufungua ubalozi Israel
Saudi Arabia imesema huenda ikafungua ubalozi wake Tel Aviv iwapo utawala haramu wa Israel utakubali kusitisha mgogoro katika eneo la Mashariki ya Kati.
Jenerali Anwar Eshki, kamanda mwandamizi wa zamani wa jeshi la Aal-Saud ameiambia kanali ya televisheni ya al-Jazeera ya Qatar kuwa, iwapo Benjamin Netanyahu, Waziri Mkuu wa utawala wa Kizayuni wa Israel atakubali mpango huo wa kusitisha mgogoro na kuwapa Wapalestina haki zao zote, basi Saudi Arabia itafungua ubalozi Tel Aviv.
Jenerali Eshki ambaye kwa sasa ni Mwenyekiti wa Kituo cha Mafunzo ya Kiistratejia na Sheria cha Mashariki ya Kati kilichoko Jeddah ameongeza kuwa, utawala wa Aal-Saud hauna haja ya kushinikiza kutengwa utawala ghasibu wa Israel katika eneo hili la Mashariki ya Kati.
Itakumbukwa kuwa, mwaka 2002, Saudia kwa mara ya kwanza ilipendekeza kuwa, iwapo utawala haramu wa Israel utawaagiza walowezi wa Kizayuni waondoke katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan na Ukanda wa Gaza, basi itazishawishi nchi zingine za Kiarabu kuutambua utawala huo dhalimu.
Hata hivyo kamanda huyo wa zamani wa jeshi la Aal-Saud na ambaye aliwahi kuwa mshauri wa Mwana Mfalme wa Aal-Saud na aliyekuwa balozi wa Saudia nchini Marekani, Bandar Bin Sultan, alikwepa kujibu swali alipotakiwa kufafanua ni kwa nini utawala wa Saudia umetuma vikosi vamizi nchini Yemen na umeshindwa kutuma vikosi katika Ukanda wa Gaza ili kuwalinda Wapalestina.
Zaidi ya watu 8,280 wameuawa wakiwemo watoto 2,236 tangu Saudia na waitifaki wake waanzishe mashambulizi ya anga dhidi ya wananchi wasio na ulinzi wa Yemen, Machi mwaka jana 2015, kwa lengo la kumrejesha madarakani rais mtoro wa nchi hiyo ya Kiarabu Abd Rabbu Mansur Hadi.