Israel yamkamata mkurugenzi katika Shirika la Wakfu Quds
Utawala wa Kizayuni wa Israel umemkamata Naibu Mkurugenzi wa Shirika la Wakfu wa Kiislamu katika mji wa Quds (Jerusalem) huku kukiwa na tetesi kuwa Wazayuni wanalenga kumuambukiza kirusi cha corona.
Kwa mujibu wa mashirika ya habari ya Palestina, wanajeshi wa utawala wa Kizayuni Jumapili usiku walishambulia nyumba ya Sheikh Najeh Bkeerat Naibu MKurugenzi wa Shirika la Wakfu wa Kiislamu mjini Quds katika kitongoji cha Sur Baher mjini Quds na kumpeleka katika kituo kimoja cha kushikilia wafungwa.
Wanaharakati wa Palestina wametahadharisha kuwa, utawala wa Kizayuni wa Israel umeanzisha kamatakamata ya watu mashuhuri wa Palestina hasa shakhsia wa kidini kwa lengo la kuwaambukiza kirusi cha corona. Aidha wanasema hivi sasa Israel iko mbioni kutekeleza njama ya kuufunga Msikiti wa Al Aqsa kwa lengo la kuuyahudisha na kuupa sura bandia ya Kiyahudi.

Hivi sasa kuna wafungwa zaidi ya 5,700 wa Palestina wanaoshikiliwa katika jela za kuogofya za utawala wa Kizayuni wa Israel na miongoni mwao kuna wanawake 250 na watoto 47.