Awamu ya pili ya ibada ya Umrah yaanza Saudia
Wizara ya Hija na Umrah Saudia imetangaza kuwa watu 250,000 wataruhusiwa kushiriki katika awamu ya pili ya ibada ya Umrah ikiwa ni katika mpango wa kuanza hatua kwa hatua ibada hiyo.
Taarifa ya wizara hiyo imesema duru ya pili ya Umrah itaanza Oktoba 18 na duru ya tatu, ambayo itawajumuisha wageni kutoka nje ya Saudia itaanza Novemba 1.
Taarifa hiyo imesema kila nchi itapangiwa idadi maalumu ya raia wake wanaoweza kushiriki katika Umrah.
Saudia ilipiga marufuku ibada ya Umrah zaidi ya miezi sita iliyopita baada ya kuibuka janga la corona. Mwaka huu pia kutokana na corona, ni idadi ndogo sana ya Waislamu walioweza kutekeleza ibada ya Hija na wote walikuwa ni wakaazi wa Saudia.
Mbali na kufika katika Msikiti Mtakatifu wa Makkah, wanaoenda Umrah pia wataruhusiwa kutembelea Al Rawdah Al Sharifa na eneo la zamani la Msikiti wa Mtume (SAW) mjini Madina.
Utawala wa Saudia umekuwa ukikosolewa kwa kutozihusisha nchi za Kiislamu duniani katika maamuzi yake kuhusu ibada za Hija na Umrah. Hatua ya Saudia ya kujichukulia maamuzi ya upande mmoja pia imekosolewa na maulamaa wa Kiislamu duniani.