Yemen: Kuanzisha uhusiano na utawala wa Kizayuni hakutadhoofisha mhimili wa muqawama
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i64210-yemen_kuanzisha_uhusiano_na_utawala_wa_kizayuni_hakutadhoofisha_mhimili_wa_muqawama
Waziri wa Mambo ya Nje wa serikali ya uokovu wa kitaifa ya Yemen amesema, hatua za wanaoamua kufanya mapatano na utawala wa Kizayuni zitashindwa tu na wala hazitadhoofisha msimamo wa mhimili wa muqawama.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Oct 24, 2020 11:26 UTC
  • Yemen: Kuanzisha uhusiano na utawala wa Kizayuni hakutadhoofisha mhimili wa muqawama

Waziri wa Mambo ya Nje wa serikali ya uokovu wa kitaifa ya Yemen amesema, hatua za wanaoamua kufanya mapatano na utawala wa Kizayuni zitashindwa tu na wala hazitadhoofisha msimamo wa mhimili wa muqawama.

Hisham Sharaf ameyasema kufuatia mapatano yaliyofikiwa kati ya Sudan na utawala haramu wa Kizayuni wa Israel ya kuanzisha uhusiano wa kawaida wa kidiplomasia.

Sharaf amesisitiza kuwa, kutangazwa makubaliano hayo ya kuanzisha uhusiano kati ya Sudan na utawala wa Kizayuni ni matokeo ya utegemezi wa kifedha na kisiasa wa Sudan kwa Saudi Arabia na Imarati, kwa sababu nchi hizo mbili zinafanya juu chini ili kujiweka karibu na serikali ya Marekani na lobi ya Kizayuni; na kutokana na Imarati kuanzisha uhusiano wa kawaida na Israel imejivua na dhima ya suala kuu la umma wa Kiislamu na Kiarabu, yaani Palestina.

Hisham Sharaf
 

Waziri wa Mambo ya Nje wa serikali ya uokovu wa kitaifa ya Yemen amebainisha kuwa, kuanzisha uhusiano wa kawaida na utawala wa Kizayuni ambayo ndiyo gharama waliyolipia wakuu wa sasa wa Sudan ili kuondolewa kwenye orodha ya ugaidi ya Marekani hakutainasua nchi hiyo na mgogoro unaoikabili hivi sasa, bali utaizidishia matatizo kwa sababu ya hatua hiyo.

Hisham Sharaf amesisitiza kuwa, kushindwa itakuwa ndio hatima ya wale wanaojaribu kuanzisha uhusiano wa kawaida na utawaala wa Kizayuni bila kuzingatia msimamo wa pamoja wa Waarabu, wala kujali haki za Wapalestina na dhulma wanazofanyiwa.../