Mfalme Salman bin Abdulaziz wa Saudi Arabia alazwa hospitalini
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i83390-mfalme_salman_bin_abdulaziz_wa_saudi_arabia_alazwa_hospitalini
Mfalme Salman bin Abdulaziz wa Saudi Arabia amelazwa katika hospitali moja mjini Jeddah kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi wa kitiba, wiki kadhaa tangu alipobadilishiwa betri ya kusaidia mapigo ya moyo.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
May 08, 2022 07:36 UTC
  • Mfalme Salman bin Abdulaziz wa Saudi Arabia alazwa hospitalini

Mfalme Salman bin Abdulaziz wa Saudi Arabia amelazwa katika hospitali moja mjini Jeddah kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi wa kitiba, wiki kadhaa tangu alipobadilishiwa betri ya kusaidia mapigo ya moyo.

Taarifa iliyotolewa leo na shirika rasmi la habari la Saudia, SPA haikutoa maelezo zaidi kuhusu hali ya afya ya mfalme huyo mzee mwenye umri wa miaka 86 wala aina ya uchunguzi na ukaguzi anaofanyiwa katika hospitali ya utaalamu maalumu ya Mfalme Faisal.

Hii ni mara ya pili katika kipindi cha miezi miwili iliyopita kwa Mfalme Salman kulazwa hospitalini. Mnamo tarehe 16 Machi, kiongozi huyo alilazwa katika hopitali Mfalme Faisal kwa ajili ya kile kilichoelezwa na ofisi ya Ufalme kuwa ni kufanyiwa uchunguzi wa kitiba na kubadilishiwa betri ya kusaidia mapigo ya moyo.

Mfalme Salman (kushoto) na mwanawe Mohammad, ambaye ndiye mrithi wa ufalme

Mwaka 2020, kiongozi huyo alifanyiwa upasuaji wa kuondoa kibofunyongo, katika anga ya ukimya iliyoibua shaka na wasiwasi kuhusu hali yake ya kiafya.

Baadhi ya taarifa, ikiwemo iliyotolewa na Mudhawi Ar-Rashid, mpinzani maarufu wa utawala wa Aal Saud inaeleza kwamba, mfalme Salman hana uwezo tena wa kutambua masuala yanayojiri kando yake.

Mara ya mwisho kiongozi huyo kuonekana hadharani ilikuwa ni katika Sala ya Idul-Fitri akiwa pamoja na mwanawe na mrithi wa ufalme Mohammad bin Salman, ambaye kiuhalisia ndiye kiongozi na mwendeshaji wa masuala ya nchi hivi sasa.../