Walowezi wa Kizayuni waendelea kuuhujumu Msikiti wa Al Aqswa
Makumi ya walowezi wa Kizayuni wameuvamia tena Msikiti wa al-Aqswa huko Palestina inayokaliwa kwa mabavu na kuuvunjia heshima msikiti huo mtakatifu.
Taarifa zaidi zinasema kuwa, katika muendelezo wa hujuma na vitendo vya chuki vya utawala wa Kizayuni wa Israel dhidi ya wananchi wa Palestina, makumi ya walowezi wa Kiyahud Jumatatu ya leo wamevamia tena msikiti mtakatifu wa al-Aqswa.
Walowezi hao wa Kizayuni wakisaidiwa na kupewa himaya kikamilifu na wanajeshi wa jeshi la Israel baada ya kuingia katika eneo la ndani la msikiti huo mtakatifu walisikika wakipiga nara dhidi ya Uislamu na Waislamu na kufanya vitendo vya kichochezi.
Katika miezi ya hivi karibuni vitendo vya hujuma na uvamizi wa walowezi wa Kizayuni katika maeneo ya Wapalestina hususan katika Msikiti wa al-Aqswa vimeongezeka mno.

Vitendo vya kuyavunjia heshima matukufu ya Kiislamu huko Palestina vinafanyika katika hali ambayo, viongozi wa nchi za Kiarabu na jamii ya kimataifa wameendelea kunyamaza kimya na kutochukua hatua zozote za maana za kukabiliana na vitendo hivyo vinavyokinzana na utu na ubinadamu.
Utawala haramu wa Kizayuni wa Israel ambao unaungwa mkono kikamilifu na Marekani na washirika wake katika hatua zake hizo haramu, umedhamiria kubadilisha muundo wa kijiografia na kidemografia wa maeneo ya Palestina; ili kuyazayunisha maeneo hayo na kuhakikisha kwamba unazihodhi na kuzidhibiti kikamilifu ardhi za wananchi madhulumu wa Palestina.