HAMAS: Viongozi wa nchi za Kiislamu amkeni kukiokoa Kibla cha Kwanza
Mkuu wa Ofisi ya Kisiasa ya Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS amewatahadharisha viongozi wa nchi za Kiislamu kuhusuu njama za kila namna za serikali mpya ya kifashisti ya Israel na kuwataka waamke kukiokoa Kibla cha Kwanza cha Waislamu.
Mashirika ya habari ya yamemnukuu Ismail Hania akitoa tahadhari hiyo jana (Jumatano) na kuzitaka nchi za Kisilamu na Kiarabu kuchukua misimamo imara na ya wazi kukabiliana na njama za utawala wa Kizayuni wa Israel.
Itamar Ben-Gvir, waziri wa usalama wa ndani wa serikali mpya ya kifashisti ya Israel, juzi Jumanne aliuvamia Msikiti wa al Aqsa ambao ni Kibla cha Kwanza cha Waislamu ikiwa ni uchokozi na fitna ya wazi kabisa dhidi ya Wapalestina na Waislamu. Ikumbukwe kuwa ni haramu kwa Wazayuni kuingia kwenye Msikiti wa al Aqsa.

Mkuu wa Ofisi ya Kisiasa ya HAMAS, Ismail Hania, pia amesema katika ujumbe wake huo kwamba, kila Muislamu ana jukumu la kuulinda na kuuhami Msikiti wa al Aqsa mbele ya njama chafu za utawala wa Kizayuni wa Israel.
Chuo Kikuu cha Kiislamu cha l Azhar cha nchini Misri nacho kimelaani vikali hatua ya waziri huyo Mzayuni mwenye misimamo ya kufurutu ada ya kuvamia Msikiti wa mtakatifu wa al Aqsa; Kibla cha Kwanza cha Waislamu.
Taarifa ya Chuo cha Kiislamu cha l Azhar cha nchini Misri imeeleza kuwa, hatua ya waziri huyo ni ya kichochezi na inaonyesha kuingiwa na woga na wahaka mkubwa utawala ghasibu wa Israel na hivi sasa unafanya njama za kutwisha matakwa yake na kutumia nguvu ya silaha kubadilisha utambulisho wa kihistoria wa mji wa Beitul-Muqaddas na Msikiti wa al Aqsa.