Uingereza: Utawala wa Kizayuni wa Israel umefanya makosa ya kutisha Ghaza
Naibu Waziri Mkuu wa Uingereza amekiri kuwa utawala wa Kizayuni wa Israel umefanya makosa makubwa na ya kutishwa kwenye Ukanda wa Ghaza.
Oliver Dowden amekiri uhakika huo katika mahojiano na shirika la habari la "Sky News" na huku akiashiria makosa makubwa yaliyofanywa na utawala wa Kizayuni kwenye Ukanda wa Ghaza ikiwa ni pamoja na kufanya mauaji ya umati ya wanawake, watoto wadogo na wananchi wa kawaida wa Palestina amesema kuwa, lazima utawala huo ghasibu wa Israel uwajibishwe kwa makosa yake hayo.
Ijapokuwa mashambulizi ya utawala wa Kizayuni katika ukanda wa Ghaza yanahesabiwa kuwa ni jinai za kivita kwa mujibu wa sheria za kimataifa, jinai ambazo zinaruhusu kufunguliwa mashitaka viongozi wa utawala wa Kizayuni katika mahakama za kimataifa, lakini upuuzaji na ucheleweshaji wa makusudi wa mambo unaofanywa kwa njia na pande tofauti hasa na nchi za Magharibi na hata Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC, umeupandisha kiburi utawala wa Kizayuni na kuuruhusu uendelee na jinai zake bila ya kiwewe wala kigugumizi dhidi ya Wapalestina wasio na hatia.
Viongozi wa utawala wa Kizayuni wa Israel wanaendeleza jinai zao hizo za kutisha kwa dhana kwamba watabakia salama kwa uungaji mkono wa kila upande wa madola ya Magharibi licha ya kufanya mauaji makubwa ya watoto wa Palestina.
Kwa mujibu wa takwimu za Wizara ya Afya ya Palestina tangu tarehe 7 Oktoba hadi hivi sasa, Israel imeshaua shahidi zaidi ya Wapalestina 33,175, na kujeruhi karibu 76,000 wengine, wengi wao wakiwa ni wanawake na watoto wadogo.