Maelfu waandamana Melbourne kulaani ziara ya rais wa 'Israel' nchini Australia
https://parstoday.ir/sw/news/world-i136584-maelfu_waandamana_melbourne_kulaani_ziara_ya_rais_wa_'israel'_nchini_australia
Maelfu ya waandamanaji wanaounga mkono Palestina walipaza sauti na kufunga barabara kadhaa mjini Melbourne, chini ya ulinzi mkali wa mamia ya polisi, wakati Rais wa utawala haramu wa Israel Isaac Herzog akihitimisha ziara yake iliyokumbwa na utata mkubwa nchini Australia.
(last modified 2026-02-13T10:36:19+00:00 )
Feb 13, 2026 10:36 UTC
  • Maelfu waandamana Melbourne kulaani ziara ya rais wa 'Israel' nchini Australia

Maelfu ya waandamanaji wanaounga mkono Palestina walipaza sauti na kufunga barabara kadhaa mjini Melbourne, chini ya ulinzi mkali wa mamia ya polisi, wakati Rais wa utawala haramu wa Israel Isaac Herzog akihitimisha ziara yake iliyokumbwa na utata mkubwa nchini Australia.

Mamlaka zilikadiria kuwa takribani waandamanaji 10,000, ambao walimtaja Herzog kuwa mhalifu wa kivita, walifunga barabara kadhaa katikati ya jiji la Melbourne kupitia mkutano mkubwa uliofanyika jioni ya Alhamisi.

Katika eneo la kibiashara la kati la Melbourne, umati mkubwa ulikusanyika nje ya moja ya vituo vikuu vya reli vya jiji hilo. Waandamanaji wengi walivaa skafu za keffiyeh na kupeperusha bendera za Palestina.

Herzog amekuwa akikabiliwa na maandamano katika kila hatua ya ziara yake ya siku nne nchini Australia, akitembelea Sydney, mji mkuu wa taifa Canberra, na Melbourne.

Hapo awali, polisi na waandamanaji walikabiliana mjini Sydney Jumatatu jioni, ambapo watu 27 walikamatwa wakati wa maandamano dhidi ya ziara ya Herzog.

Polisi walitumia gesi ya machozi na pilipili kuwatawanya waandamanaji katika eneo la biashara la kati la jiji hilo.

Waandamanaji wamenukuu Tume ya Uchunguzi ya Umoja wa Mataifa ambayo mwaka jana ilihitimisha kuwa Israel imefanya vitendo vinavyofikia kiwango cha mauaji ya kimbari huko Gaza, na kusema kuwa maafisa wakuu wa Israel, akiwemo Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu na Rais Herzog, walichochea vitendo hivyo.

Herzog anafanya ziara ya Australia wiki hii kufuatia mwaliko wa Waziri Mkuu wa Australia Anthony Albanese, baada ya tukio la ufyatuaji risasi tarehe 14 Desemba katika hafla ya Hanukkah katika eneo la Bondi Beach, Sydney, lililosababisha vifo vya watu 15.

Ziara hiyo imezua hasira miongoni mwa raia wengi wa Australia, wanaomshutumu Herzog kwa kushiriki au kunyamazia vifo vya idadi kubwa ya raia katika Ukanda wa Gaza unaozingirwa.

Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC) ilitoa hati ya kukamatwa dhidi ya Netanyahu na aliyekuwa waziri wake wa vita tarehe 21 Novemba 2024, kwa kuhusika katika uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya ubinadamu huko Gaza, ambako zaidi ya watu 72,000 wameuawa tangu Oktoba 2023, wengi wakiwa ni wanawake na watoto.

Ripoti zinaonyesha kuwa ICC pia ilikuwa ikitafuta kutoa hati nyingine za kukamatwa dhidi ya maafisa wa Israel, kuhusiana na mashambulizi yanayoendelea ya nguvu kupita kiasi dhidi ya Wapalestina katika Ukanda wa Gaza unaozingirwa.