Ushindi wa Trump wawafanya raia wa Marekani kuandamana kuwaunga mkono Waislamu
Raia wa jimbo la Texas nchini Marekani wamefanya maandamano kutangaza uungaji wao mkono kwa jamii ya Waislamu wa nchi hiyo kufuatia ushindi wa Donald Trump, rais mteule.
Mtandao wa habari wa TWC News umeripoti kuwa, wakazi wasio Waislamu wa mji wa Austin jimboni hapo waliandamana Ijumaa ya jana mbele ya msikiti wa eneo la Nueces kuwaunga mkono Waislamu na kuonyesha radiamali yao juu ya ushindi wa Trump katika uchaguzi wa rais wa hivi karibuni nchini humo.
Katika maandamano hayo, Wamarekani hao wasio Waislamu walibeba mabango na maberamu yaliyokuwa na jumbe tofauti baadhi zikisema, 'urafiki utashinda chuki' na 'sisi sote ni watu wa taifa moja.' Arian Hom, mmoja wa washiriki wa maandamano hayo alinukuliwa akisema kuwa, Wamarekani wote wanatakiwa kuwaunga mkono Waislamu ili kuwafanya nao waweze kuhisi amani na usalama.
Naye Mohammed Omar Ismail, imamu wa jamaa wa msikiti wa mji wa Austin amesema kuwa, uungaji mkono wa raia hao wasio Waislamu kwa jamii ya Waislamu na katika kipindi hiki ambacho kinatawala siasa za kibaguzi nchini, ni jambo muhimu sana. Hayo yanajiri kufuatia ushindi wa Donald Trump, aliyetangazwa mshindi tarehe nane ya mwezi huu, ambaye katika kipindi cha kampeni zake kwa mara kadhaa alitangaza wazi kuwa, endapo atashinda uchaguzi, atawazuia Waislamu kuingia nchini humo.
Inafaa kuashiria kuwa, tangu mfanyabiashara huyo mashuhuri atangazwe kuwa mshindi, vitendo vya ubaguzi nchini Marekani vimeongezeka. Aidha maandamano na machafuko ya kupinga ushindi wa Trump yameendelea kushuhudiwa katika maeneo mengi ya nchi hiyo huku karibu watu 20 wakiripotiwa kuuawa na wengine wengi kujeruhiwa.