Dec 23, 2016 06:55 UTC
  • Iran na Kyrgyzstan zasaini hati tano za mapatano ya ushirikiano

Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran leo Ijumaa amekutana na Rais Almazbek Atambayev wa Kyrgyzstan katika ikulu ya rais huyo mjini Bishkek na kufanya mazungumzo kuhusu kuimarisha uhusiano wa pande pamoja na masuala mbalimbali ya kieneo na kimataifa.

Nchi mbili za Iran na Kyrgyzstan zimesaini hati tano za mapatano ya ushirikiano kati yao baada ya marais wa nchi hizo kufanya mazungumzo ya pande mbili katika ikulu ya Bishkek. Hati hizo tano za ushirikiano zimesainiwa mbele ya Marais wa Iran na mwenyeji wake wa Kyrgyzstan.

Maafisa wa Iran na Kyrgyzstan wamesaini hati tano za mapatano ya ushirikiano katika nyanja za mawasiliano na teknolojia ya habari, kupambana na uzalishaji, magendo na matumizi ya mihadarati, kubadilishana masuala ya kiutamaduni na sanaa, taarifa za vyombo vya habari na utalii, afya na tiba, na kushirikiana pia katika nyanja ya kijaamii na kazi. Nchi mbili hizo zimesaini mapatano hayo ya ushirikiano ili kuimarisha uhusiano na mashirikiano kati ya pande mbili. 

Rais Rouhani wa Iran (kulia) akiwa ikulu huko Bishkek na Rais wa Kyrgyzstan 

Katika ziara hii ya Rais wa Iran huko Bishkek, kumetolewa pia taarifa ya pamoja kuhusu mpango wa ushirikiano wa muda mrefu kati ya Iran na Kyrgyzstan kuanzia mwaka 2016 hadi 2026. Rais Hassan Rouhanii jana usiku aliwasili Bishkek mji mkuu wa Kyrgyzstan akiwa katika marhala na hatua ya mwisho ya ziara yake ya kutembelea nchi kadhaa ambako alilakiwa rasmi katika uwanja wa ndege na Rais Almazbek Atambayev wa nchi  hiyo. 

Tags