Asilimia kubwa ya Wamarekani wanapinga kuzuiwa Waislamu kuingia US
Matokeo ya utafiti wa maoni yanaonyesha kuwa asilimia kubwa ya raia wa Marekani wanapinga marufuku ya kuzuiwa Waislamu kuingia nchi hiyo.
Matokeo ya utafiti uliofanywa na taasisi ya Sera za Umma kwa kuwahoji raia wa Marekani yameonyesha kwamba asilimia 65 ya Wamarekani wanapinga marufuku ya Rais Trump ya kuwazuia Waislamu kuingi nchini humo. Kwa mujibu wa ripoti hiyo, asilimia 26 ya walioshiriki utafiti huo, wameunga mkono marufuku hiyo huku asilimia tisa wakisema kuwa hawajui la kusema.
Licha ya kuendelea kuenezwa propaganda za chuki dhidi ya Uislamu katika jamii ya Marekani kunakofanywa na vyombo mbalimbali vya habari, bado inaonekana kuwa propaganda hizo hazijawa na taathira yoyote ile, na badala yake raia wengi wa nchi hiyo wameendelea kuwa na mtazamo chanya kuihusu dini hiyo ya mbinguni na wafuasi wake.
Hii ni katika hali ambayo mapema kabla ya hapo Rais Donald Trump wa Marekani alitia saini marufuku ya kuwazuia raia wa nchi saba za Kiislamu ikiwemo Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kuingia Marekani. Marufuku hiyo ambayo iliwekwa kisiasa, ilikabiliwa na wimbi kubwa la malalamiko ndani na nje ya Marekani.