UN yataka kusitishwa mashambulizi ya Saudia dhidi ya Yemen
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ametoa wito wa kusitishwa mashambulizi ya anga na nchi kavu yanayoendelea kufanywa na Saudi Arabia na washirika wake dhidi ya watu wa Yemen na kuanza tena kuingizwa bidhaa za kibiashara nchini humo.
Antonio Guterres ametahadharisha kuwa, mamilioni ya watoto, wanawake na wanaume wa Yemen wanakabiliwa na hatari ya baa la njaa, maradhi na kifo kutokana na mashambulizi na kuzingirwa nchi hiyo.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amesema ana wasiwasi mkubwa kuhusu kushadidi vita nchini Yemen na amezitaka pande zote kusitisha mashambulizi ya anga na nchi kavu.
Vyombo vya habari nchini Yemen vimeripoti kuwa Saudi Arabia na washirika wake wamezidisha mashambulizi ya anga dhidi ya mji mkuu wa Yemen, San'aa baada ya rais wa zamani wa nchi hiyo, Abdullah Saleh kutangaza kuwa, haiunge tena mkono harakati ya wananchi ya Ansarullah.
Maelfu ya raia, wengi wao wakiwa watoto na wanawake, wameuawa na mamilioni ya wengine kuwa wakimbizi kutokana na mashambulizi yanayoendelea kufanywa na Saudi Arabia na washirika wake dhidi ya Yemen.
Umoja wa Mataifa umetangaza vita vya Yemen na mashambulizi ya Saudi Arabia dhidi ya watu wa nchi hiyo kuwa ni maafa makubwa zaidi ya karne ya sasa.