Kashfa za ngono zaendelea kumwandama Rais wa Marekani
Vyombo vya habari vya Marekani vimeripoti kuwa, kashfa ya mahusiano haramu ya ngono inayomwandama Rais Donald Trump wa nchi hiyo inazidi kupamba moto na kwamba kiongozi huyo ameamua kumwajiri wakili mashuhuri kwa ajili ya kujinasua katika kinamasi hicho.
Televisheni ya ABC News imeripoti kuwa, timu ya kisheria ya Donald Trump imemwajiri wakili mpya anayejulikana kwa jina la Lawrence Rosen mjini New York ili kuweza kumuokoa Rais wa nchi hiyo katika kashfa ya utovu wa maadili wa kuwa na uhusiano haramu wa kingono na mchezaji wa filamu za ufuska, Stephanie Gregory Clifford.
Mwanamke huyo anayejulikana kwa jina la kisanii la Stormy Daniels, amewasilisha mashtaka mahakamani kwamba mwaka 2006 yaani mwaka mmoja baada ya Trump kumuoa Melania, alifanya maingiliano haramu ya kingoni na kiongozi huyo wa Marekani.
Awali gazeti la Wall Street Journar lilikuwa limefichua kwamba, Donald Trump alimpa Clifford dola laki moja na 30 elfu kupitia kwa wakili wake ili kumnyamazisha asifichue suala hilo wakati wa kampeni za uchaguzi wa rais wa Marekani mwaka 2016.
Clifford amesema wakili wa Rais Donald Trump wa Marekani alifanya jitihada kubwa za kumnyamazisha hata kwa kutumia vitisho.