"Iran haiwezi kufanya mazungumzo na Trump kidhabi"
Mchambuzi mmoja wa Kimarekani amesema kuwa Iran haiwezi kufanya mazungumzo na serikali kidhabi ya Donald Trump ambayo haioneshi nia yoyote nzuri katika mazungumzo.
Rodney Martin, mchambuzi maarufu wa masuala ya kisiasa wa nchini Marekani ameliambia shirika la habari la Tasnim kuwa, matamshi ya viongozi wa nchi hiyo kuhusiana na Iran hayana ukweli kwani Marekani haifanya mambo yake kama nchi ya kawaida bali imeanzisha vita vya kila namna ili kujionyesha kuwa ndiyo nchi pekee yenye nguvu duniani suala ambalo haliwezi kukubaliwa hata kidogo na mataifa huru duniani.
Amesema, rais wa Marekani, Donald Trump, Mike Pompeo, waziri wa mambo ya nje wa nchi hiyo na John Bolton, mshauri wa usalama wa taifa wa Marekani wote wasiwasi wao mkubwa ni kulinda manufaa ya Israel na hawashughulishwi hata kidogo na amani na usalama wa kimataifa.
Vile vile amesema, moja ya sababu kuu za hamaki za Washington ni kwamba Iran katika miaka ya huko nyuma iliitimua Marekani nchini humo na sasa hivi White House haina ushawishi wowote katika masuala ya ndani ya Iran.
Mtaalamu huyo wa masuala ya kisiasa wa Marekani amegusia pia jinsi Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ilivyosimama imara kukabiliana na njama na mashinikizo ya Marekani na kuongeza kuwa, Iran haiwezi kufanya mazungumzo na viongozi wa Marekani ambao wanaonesha wazi kuwa hawana nia njema.