Pompeo adai kampuni ya Huawei ya China inakiuka haki za binadamu
Katika kuendelea prppaganda chafu za Washington dhidi ya Beijing, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani amedai kuwa kampuni kubwa ya China ya Huawei inakiuka haki za binadamu.
Mike Pompeo ambaye anaongoza kampeni za serikali ya Rais Donald Trump wa Marekani dhidi ya China amesema Washingtion itawanyima viza wafanyakazi wa makampuni ya teknolojia ya China kama ile ya Huawei.
Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani ameandika katika ukurasa wake wa Twitter kuwa kampuni ya Huawei ya China inazipatia teknolojia tawala ambazo Washington inadai kuwa zinakiuka haki za binadamu.
Karibu miaka miwili sasa ambapo serikali ya Marekani imeiwekea vikwazo kampuni hiyo ya Huawei ya China kwa madai kuwa, inafanya ujasusi kwa maslahi ya China na kwamba kampuni hiyo ni tishio kwa usalama wake wa taifa.
Serikali ya Uingereza pia imeiunga mkono Marekani dhidi ya Huawei ambapo hivi karibuni iliamuru kuondolewa kikamilifu vifaa vya Huawei katika mtandao wa G5 wa Uingereza hadi kufikia mwishoni mwaka 2027.
Wachina wanaamini kuwa, sababu kuu iliyoifanya Marekani idai kuwa kampuni ya Huawei inafanya ujasusi kwa maslahi ya China ili kulinda maslahi ya makampuni shindani ya Marekani na kuzuia ushawishi wa bidhaa za Huawei katika masoko ya ndani ya Marekani.