Umoja wa Ulaya: Hatutaitambua serikali ya Taliban Afghanistan
Mkuu wa Kamisheni ya Umoja wa Ulaya amesisitiza kuwa umoja huo hautaitambua serikali ya kundi la Taliban inayotawala nchini Afghanistan.
Ursula von der Leyen amesema, kuna ulazima wa kuchukua hatua za kuzuia msambaratiko wa kiuchumi na kijamii unaokaribia kutokea nchini Afghanistan lakini akasisitiza pia kwamba Umoja wa Ulaya hauitambui serikali mpya iliyoko Afghanistan iliyoundwa kwa kutumia njia za mabavu.
Matamshi ya Bi Ursula von der Leyen yanatolewa katika hali ambayo, mazungumzo baina ya wajumbe wa Taliban na wawakilishi wa Marekani na Ulaya yameanza jana Jumamosi katika mji mkuu wa Qatar, Doha.
Tareha 7 Septemba mwaka huu, Taliban ilitangaza kuunda serikali ya muda nchini Afghanistan.
Miaka 20 iliyopita, Marekani na Uingereza pamoja na waitifaki wao, kwa kutumia mwavuli wa shirika la kijeshi la NATO waliishambulia na kuivamia kijeshi Afghanistan kwa kisingizio cha kupambana na ugaidi. Lakini baada ya miongo miwili ya kuikalia kwa mabavu nchi hiyo, kusababisha uharibifu mkubwa, kutumia dola bilioni 2,313 mbali na askari wake wapatao 2,500 waliouawa, hatimaye mwezi Agosti mwaka huu ilitimka na kuihama Afghanistan huku ikiacha doa na rekodi nyingine chafu ya uingiliaji wake wa masuala ya ndani ya nchi za eneo la Asia Magharibi.../