Putin aongeza idadi ya wanajeshi wa Russia, wapindukia milioni 1
https://parstoday.ir/sw/news/world-i87438-putin_aongeza_idadi_ya_wanajeshi_wa_russia_wapindukia_milioni_1
Rais Vladimir Putin wa Russia amesaini dikrii ya kuongeza idadi ya wanajeshi wa nchi hiyo, huku operesheni maalumu ya kijeshi ya Moscow dhidi ya Ukraine ikiingia mwezi wa saba.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Aug 26, 2022 02:41 UTC
  • Putin aongeza idadi ya wanajeshi wa Russia, wapindukia milioni 1

Rais Vladimir Putin wa Russia amesaini dikrii ya kuongeza idadi ya wanajeshi wa nchi hiyo, huku operesheni maalumu ya kijeshi ya Moscow dhidi ya Ukraine ikiingia mwezi wa saba.

Dikrii hiyo iliyochapishwa katika tovuti ya Ikulu ya Kremlin inasema kuwa, jeshi la Russia linaongeza idadi ya vikosi vyake kwa askari 137,000, na sasa litakuwa na jumla ya wanajeshi milioni 1.15.

Kwa mujibu wa dikrii hiyo iliyosainiwa jana Alkhamisi na Rais Putin, jeshi la Russia litakuwa na askari zaidi ya milioni mbili kufikia Januari mwaka ujao 2023.

Mwaka 2017, Rais Putin alisema idadi ya askari wa nchi hiyo ilikuwa milioni 1.9, wakiwemo wanajeshi zaidi ya milioni moja wa vikosi mbalimbali vya nchi hiyo. 

Rais Putin

Ingawaje dikrii iliyosainiwa Alkhamisi haijaeleza sababu ya Moscow kuongeza idadi ya wanajeshi wake, lakini hatua hiyo imekuja wakati huu ambapo vikosi vya Russia vinafanya jitihada za kudhibiti maeneo ya mashariki ya Ukraine.

Moscow ilianzisha operesheni maalumu nchini Ukraine mnamo Februari 24, kwa lengo la kuizuia nchi hiyo isiendelee kujitanua kuelekea upande wa mashariki, kwa madhara ya usalama wa Russia.