Jumamosi, 10 Novemba, 2018
Leo ni Jumamosi tarehe Pili Mfunguo Sita Rabiul Awwal 1440 Hijria ambayo inasadifiana na tarehe 10 Novemba 2018 Miladia.
Siku kama ya leo miaka 810 iliyopita kwa mujibu wa kalenda ya Hijria, aliaga dunia Ibn Athir Jazari, mwanahistoria, mtaalamu wa fasihi na mpokezi mkubwa wa hadithi. Ibn Athir alizaliwa mwaka 555 Hijria huko Iraq na kujifunza taaluma mbalimbali. Alipata umashuhuri katika masuala ya lugha na fasihi ya Kiarabu. Kitabu maarufu zaidi cha Ibn Athir ni al Kamil fi Tarikh. Kitabu kingine cha mwanazuoni huyo mkubwa wa Kiislamu ni Usudul Ghabah Fi Ma'rifatis Sahabah ambacho kinaeleza wasifu wa masahaba 7500 wa Mtume Muhammad (saw). ***
Miaka 535 iliyopita katika siku kama ya leo ya tarehe 10 Novemba, alizaliwa Martin Luther mpigania mageuzi ya kidini wa Kijerumani. Luther alikuwa padri wakati akiwa kijana. Mitazamo ya Martin Luther kuhusuiana na dini ya Kikristo ilitofautiana na baadhi ya mitazamo ya Papa na viongozi wa ngazi ya juu wa kanisa na kuanzia mwaka 1517, Luther alidhihirisha mapambano na upinzani wake dhidi ya dhulma na ukandamizaji wa kanisa. Martin Luther alipinga waziwazi agizo la Papa wa Kanisa Katoliki kwa kuifasiri Injili kwa lugha ya Kijerumani na akaanzisha harakati ya kiprotestanti dhidi ya kanisa hilo. ***
Tarehe 10 Novemba 1912 yaani miaka 106 iliyopita, Morocco iliwekwa chini ya himaya ya wakoloni wa Ufaransa na Uhispania. Uislamu uliingia Morocco mwishoni mwa karne ya 7 na nchi hiyo ikapewa jina la Maghrib kutokana na ardhi yake kuwa upande wa magharibi mwa ardhi ya nchi za Kiislamu. ***
Siku kama ya leo miaka 65 iliyopita, Dakta Sayyid Hussein Fatimi Waziri wa Mambo ya Nje wa serikali ya Dakta Muhammad Musaddiq aliuawa kwa kupigwa risasi na vibaraka wa utawala wa Shah nchini Iran. Dakta Fatimi kabla ya hapo alikuwa amehukumiwa kunyongwa na mahakama moja ya kijeshi ya kimaonyesho ya utawala wa Shah huku akiwa mgonjwa sana. Baada ya mapinduzi ya Marekani na Ui9ngereza ya tarehe 28 Mordad mwaka 1332 Hijria Shamsiya hapa nchini na baada ya kujiuzulu Dakta Musaddiq, Dakta Sayyid Hussein Fatimi alikuwa akisakwa na vibaraka wa utawala wa Shah na alikuwa akiishi kwa kujificha. Alikamatwa na kunyongwa katika siku kama ya leo. ***
Miaka 54 iliyopita katika siku kama ya leo, Leonid Brezhnev aliteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Chama cha Kikomonisti cha Urusi ya zamani na hivyo kushika hatamu za kukiongoza chama hicho. Mwaka 1931, Brezhnev alijiunga na kuwa mwanachama wa chama hicho cha Kikomonisti. Mashambulizi ya Urusi dhidi ya Czechoslovakia na kuvamiwa kijeshi Afghanistan vilifanyika katika zama zake. ***
Na katika siku kama ya leo miaka 43 iliyopita, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilitoa azimio nambari 3379 lililoutambua uzayuni (Zionism) kuwa ni aina fulani ya ubaguzi wa kizazi. Azimio hilo lilitoa pigo kubwa kwa utawala wa Kizayuni wa Israel na kufichua utambulisho halisi wa utawala huo. Azimio hilo la Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa liliikasirisha sana Israel na waungaji mkono wa utawala huo wa kibaguzi hususan Marekani. Tofauti na mafundisho ya Kiyahudi, fikra za uzayuni ambazo zilianzishwa mwishoni mwa karne ya 19 zinawatambua wafuasi wa dini hiyo kuwa ni ndio kizazi bora zaidi ya wengine wote duniani. Kwa mujibu wa fikra hiyo, Wazayuni wa Israel wanawatambua watu wa Palestina kuwa ni kizazi duni na hakiri zaidi na kwa sababu hiyo wanawakandamiza, kuwaua na kuwafukuza katika makazi na maeneo yao. ***