Feb 03, 2019 01:23 UTC
  • Jumapili Februari 3

Leo ni Jumpilii tarehe 27 Jamadul-Awwal 1440 Hijiria, sawa na tarehe tatu Fenruari 2019 Miladia.

Siku kama ya leo miaka 551 iliyopita, alifariki dunia mvumbuzi wa mashine ya uchapishaji, Johannes Gutenberg. Mvumbuzi huyo alizaliwa nchini Ujerumani lakini alihamia Strasbourg, Ufaransa na akaanza kujishughulisha na kazi za kiufundi. Mwaka 1443 au 1444 Gutenberg alifanikiwa kutengeneza mashine ya uchapishaji na kupiga hatua muhimu katika uchapishaji na uenezaji wa elimu na maarifa kati ya wanadamu. Katika zama zake, Johannes Gutenberg pia alichapisha kitabu cha Biblia maarufu kwa jina la' Gutenberg Bible.'

Johannes Gutenberg

Siku kama ya leo miaka 262 iliyopita alifariki dunia Abdul-Karim Bin Ahmad Halabi, Mtaalamu wa Hadithi wa Kiislamu. Ahmad Halabi alikuwa kati ya wataalamu wa hadithi wa zama zake mjini Halab (Aleppo), Syria ya leo. Msomi huyo alisoma elimu za fiqhi, usulu fiqhi, tafsiri ya Qur'ani, hadithi na elimu nyingine za zama zake kutoka kwa baba yake na maulama wengine wa zama zake. Hata hivyo baadaye alipatwa na maradhi ya upofu, ingawa hakupoteza irada yake ya kutafuta na kufundisha elimu ya hadithi. Abdul-Karim Bin Ahmad Halabi ameacha athari nyingi ikiwa ni pamoja na kitabu cha 'Ad'iyatus-Safar.'

Abdul-Karim Bin Ahmad Halabi

Siku kama ya leo miaka 189 iliyopita, Ugiriki ilipata uhuru wake kutoka kwa utawala wa Othmania. Ugiriki ambayo kijiografia ipo kusini mashariki mwa Ulaya ni moja kati ya nchi zenye tamaduni kongwe zaidi duniani. Mwaka 338 kabla ya kuzaliwa Nabii Isa (a.s), mfalme wa Macedonia aliivamia Ugiriki na karne moja baadaye nchi hiyo ikawa chini ya mamlaka ya utawala wa Roma na baadaye Roma ya Mashariki. Katika kipicdi chote cha karne ya 19, Ugiriki ilishuhudia mapigano na vurugu za ndani na nje. Hatimaye katika siku kama ya leo nchi hiyo ikajipatia uhuru.

Bendera ya Ugiriki

Siku kama ya leo miaka 104 iliyopita, Mfereji wa Suez uliokuwa ukidhibitiwa na Uingereza, ulishambuliwa na vikosi vya majeshi ya Ujerumani na utawala wa Othmaniya katika Vita vya Kwanza vya Dunia. Udhibiti wa mfereji huo wa Suez ulikuwa na umuhimu mkubwa kwa pande mbili zilizokuwa zikipigana katika Vita vya Kwanza vya Dunia kutokana na ukweli kwamba, mfereji huo ndio unaounganisha Bahari ya Mediterania na Bahari Nyekundu. Uingereza ambayo haikuwa tayari kupoteza makoloni yake ya Asia, ilipigana vikali na majeshi ya Ujerumani na utawala wa Othmaniya na kupata ushindi. Mfereji wa Suez uliendelea kudhibitiwa na Uingereza hadi ulipotaifishwa na kiongozi wa Misri Gamal Abdul Nasir hapo mwaka 1956.

Mfereji wa Suez

Siku kama ya leo miaka 95 iliyopita, Woodrow Wilson Rais wa 28 wa Marekani alifariki dunia. Woodrow Wilson alizaliwa 1913 na akiwa na umri wa miaka 57 alichukua hatamu za uongozi wa Marekani. Kama walivyokuwa marais waliomtangulia wa Marekani, na yeye alikita zaidi katika kuingilia masuala ya ndani ya Amerika ya Kati. Kipindi cha urais wa Woodrow Wilson kilitawaliwa na uingiliaji na uvamizi wa kijeshi dhidi ya maeneo mbalimbali duniani. Nusu ya kipindi cha utawala wa Woodrow Wilson, kilishuhudia Marekani ikishughulishwa na vita. Nchi zilizoshambuliwa kijeshi na Marekani katika uongozi wa Rais Woodrow Wilson ni Haiti, Guatemala, Dominican na Cuba.

Woodrow Wilson

Siku kama ya leo, tarehe 14 Bahman 1357 Hijria Shamsia yaani miaka 40 iliyopita, wananchi wa Iran walipokuwa katika sherehe na shamrashamra za kumkaribisha nchini Imam Khomeini akitokea uhamishoni nje ya nchi, Imam alizungumza na waandishi habari akieleza misimamo ya mfumo ujao wa utawala wa Kiislamu hapa nchini na kutangaza kuwa kwa ushirikiano wa wananchi angeunda serikali ya mpito ya mapinduzi muda mfupi baadaye. Imam Khomeini alitangaza kuwa serikali hiyo ya mpito ingekuwa na jukumu la kutayarisha kura ya maoni ya Katiba mpya ya Iran. Vile vile alimtahadharisha Shapour Bakhtiar Waziri Mkuu wa serikali ya wakati huo ya Shah kwamba, iwapo angeendelea kuwakandamiza wananchi angetangaza vita vya jihadi. Imam Khomeini vile vile alilitaka jeshi lijiunge na mapambano ya wananchi dhidi ya utawala wa Shah. Wakati huohuo ilitangazwa kwamba, Wamarekani elfu 35 walikuwa wamekwishaondoka katika ardhi ya Iran na kwamba wengine elfu 10 walikuwa mbioni kuondoka nchini.

Imam Khomeini (MA)

Na siku kama ya leo miaka 9 iliyopita  kwa mujibu wa kalenda ya Hijria Shamsia, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ilirusha kwa mafanikio roketi ya kwanza ya kubebea satalaiti angani iliyojulikana kwa jina la Omid. Miaka iliyofuata Iran ilituma viumbe hai angani kwa mafanikio ikiwa ni pamoja na kobe na tumbili na hatua hiyo kuiingiza Iran katika klabu ya nchi zenye teknolojia ya anga za mbali tena katika kipindi hicho cha vikwazo vikali vya kiuchumi vya nchi za Magharibi.