Jumatatu, Desemba 21, 2020
Leo ni Jumatatu tarehe 6 Mfunguo Nane Jamadil-Awwal 1442 Hijria mwafaka na tarehe 21 Desemba 2020 Miladia.
Siku kama ya leo miaka 1028 iliyopita kwa mujibu wa kalenda ya Hijria, aliaga dunia Abu Said Muhammad bin Abdul-Jalil Sistani mwanahisabati mahiri na mashuhuri wa Kiislamu. Alibobea katika nyuga za hisabati, jiometri na nujumu na alihesabiwa kuwa mwalimu hodari wa taaluma hizo. Abu Said Sistani alikuwa akialifu kitabu katika kila taaluma aliyokuwa akiikosomea. Kitabu cha Jamiu Shahi katika hisabati ni miongoni mwa athari muhimu za msomi huyu wa Kiislamu. ***
Katika siku kama ya leo miaka 196 iliyopita, alifariki dunia tabibu na mtaalamu wa masuala ya ardhi wa Uingereza, James Parkinson. Alijifunza tiba kwa baba yake na alikuwa wa kwanza kueleza kwamba ugonjwa wa kidole tumbo (appendix) unaweza kusababisha kifo. Parkinson aligundua ugonjwa wa kutetemeka au kukakamaa (Parkinson kwa kimombo) na namna unavyotokea. Kwa sababu hiyo ugonjwa huo ulipewa jina la tabibu huyo. Dalili za ugonjwa huo ni kama vile kutetemeka sana na kwa muda mrefu kwa ulimi, kichwa na mikono na kushindwa kuvuta miguu wakati wa kutembea hususan katika kipindi cha uzeeni na pia kukakamaa misuli katika sehemu yoyote ya mwili. Ugonjwa wa Parkinson unasababishwa na baadhi ya matatizo katika ubongo na hadi kufikia sasa hakuna dawa mujarabu iliyopatikana kwa ajili ya kutibu maradhi hayo. ***
Siku kama ya leo miaka 32 iliyopita, watu 270 walipoteza maisha yao baada ya ndege ya abiria ya Marekani kuripuka katika anga ya Lockerbie huko Scotland. Marekani na Uingereza ziliwatuhumu raia wawili wa Libya kuwa ndio waliotega bomu katika ndege hiyo. Kufuatia mashinikizo ya nchi mbili hizo, mwaka 1992, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa liliiwekea vikwazo vya mafuta, anga na kijeshi nchi ya Libya, kwa tuhuma za kuwaficha Walibya hao. Hata hivyo kufuatia makubaliano kati ya Washington na serikali ya Tripoli, mwaka 1999 watuhumiwa hao walikabidhiwa kwa Mahakama ya Kimataifa ya Jinai yenye makao yake makuu mjini The Hague, Uholanzi ambapo baada ya kesi hiyo mmoja kati ya watuhumiwa hao aliachiliwa huru baada ya kutopatikana na hatia, na wa pili alihukumiwa kifungo cha maisha jela. ***
Na miaka 7 iliyopita katika siku kama ya leo, Ahmed Asmat Abdel-Meguid, Katibu Mkuu wa zamani wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu aliaga dunia akiwa na umri wa miaka 90. Ahmed Asmat Abdel-Meguid aliyekuwa mwanadiplomasia wa Kimsri alizaliwa mwaka 1923 katika mji wa Alexandria nchini Misri. Aliongoza Jumuiya ya Nchi za Kiarabu kuanzia mwaka 1991-2001. Kabla ya kuchaguliwa kushika wadhifa huo, Ahmed Asmat Abdel-Meguid alikuwa Waziri wa Mashauuri ya Kigeni wa Misri kuanzia 1984 hadi 1991. Aidha mwaka 1985 alishika wadhifa wa Naibu Waziri Mkuu. Kadhalika Ahmed Asmat Abdel-Meguid aliwahi kuwa balozi wa Misri nchini Ufaransa na mwakilishi wa nchi hiyo katika Umoja wa Mataifa. ***