Apr 07, 2021 22:08 UTC
  • Alkhamisi tarehe 8 Aprili mwaka 2021

Leo ni Alkhamisi tarehe tarehe 25 Shaabani 1442 Hijria sawa na tarehe 8 Aprili mwaka 2021.

Siku kama ya leo miaka 162 iliyopita, alizaliwa Edmund Husserl, msomi wa hisabati na falsafa wa nchini Austria. Husserl alielekea Ujerumani kwa ajili ya kujiendeleza kielimu ambapo akiwa huko alifanikiwa kufikia daraja ya Uprofesa. Kadhalika Edmund Husserl alifanya utafiti mwingi kuhusiana na elimu ya falsafa. Husserl alitambuliwa pia kuwa mwasisi wa kanuni ya Phenomenology katika falsafa, ambayo ilikuwa na taathira kubwa kwa wanafalsafa wa Kimagharibi. Aidha aliamini kwamba lazima falsafa iambatane na hisabati, kama ambavyo aliamini kwamba dunia lazima iwe nzuri na ya kuvutia. Ameacha athari mbalimbali ikiwemo 'Falsafa ya Hisabati' 'Uchunguzi wa Kimantiki' na vitabu vingine.

Edmund Husserl

Siku kama ya leo miaka 51 iliyopita, ndege za kijeshi za utawala haramu wa Israel ziliishambulia shule ya msingi ya Bahrul Baqar iliyoko umbali wa kilomita 80 kaskazini mwa mji wa Cairo. Katika mashambulizi hayo ya kutisha watoto 46 waliokuwa wakisoma shuleni hapo waliuawa. Mashambulizi hayo ya kikatili yaliibua hasira ya watu katika nchi mbalimbali duniani. Kwa muda wa miezi mitatu ya awali ya mwaka 1970 ndege za utawala haramu wa Israel ziliyashambulia maeneo ya kiraia huko kaskazini mashariki mwa Misri. Tarehe 12 Februari mwaka huohuo Wazayuni pia walikishambulia kiwanda kimoja katika eneo hilo na kuua pamoja na kuwajeruhi wafanyakazi 168. Kadhalika Wazayuni waliwaua watu 12 katika mashambulizi dhidi ya mji wa al-Mansura ulio kaskazini mashariki mwa nchi hiyo tarehe 31 mwezi Machi mwaka huohuo wa 1970.

Jinai za utawala wa Kizayuni wa Israel

Siku kama ya leo miaka 41 iliyopita utawala wa Baathi nchini Iraq uliwaua Shahidi Sayyid Muhammad Baqir-Sadr na dada yake Bintul Huda. Akiwa mtoto Sadr alijifunza Qur'ani Tukufu na elimu nyingine za kidini na akafikia daraja ya ijtihad akiwa kijana. Alikuwa mmoja wa walimu wakubwa wa chuo cha kidini mjini Najaf Iraq kiasi kwamba, nadharia zake katika elimu ya Usulu Fiqhi zilipewa umuhimu mkubwa na wasomi wengine wa Kiislamu. Msomi huyu aliyekuwa na uelewa na uwezo wa hali ya juu wa kielimu, aliuarifisha Uislamu kwa njia sahihi. Kwa kipindi kifupi Ayatullah Sadr aligeuka na kuwa kiongozi wa kifikra na kisiasa wa wananchi wa Iraq na kuyapa mwelekeo mpya mapambano ya wananchi wa Iraq. Baada ya muda fulani utawala wa nchi hiyo ambao ulihisi hatari kutokana na harakati za Ayatullahi Sadr ulimtia mbaroni na kisha kumuua shahidi mwanazuoni huyo mashuhuri pamoja na dada yake, licha ya malalamiko makubwa ya maulama na wananchi Waislamu wa Iraq. Miongoni mwa vitabu vya msomi huyo ni pamoja na kitabu kiitwacho "Hamasa ya Nuru", "Falsafa Yetu", "Mwanadamu wa Leo na Matatizo ya Kijamii", na "Ukhalifa wa Mwanadamu na Ushuhuda wa Mitume."

Shahidi Sayyid Muhammad Baqir-Sadr

Na miaka 8 iliyopita katika siku kama ya leo Margaret Hilda Thatcher, Waziri Mkuu wa zamani wa Uingereza alifariki dunia. Margaret Thatcher alikuwa mwanachama wa Chama cha Wahafidhina nchini Uingereza ambapo mwaka 1975 alichaguliwa kuwa kiongozi wa chama hicho. Mwaka 1990 alikuwa kiongozi wa Chama cha Wahafidhina nchini Uingereza na Waziri Mkuu wa nchi hiyo. Thatcher ndiye mwanamke wa kwanza wa Uingereza kushikilia uongozi wa chama na Uwaziri Mkuu kwa pamoja. 

Margaret Hilda Thatcher