Miripuko pacha ya mabomu yaua watu kadhaa mjini Mogadishu, Somalia
Kwa akali watu wanane wameuawa na wengine kadhaa wamejeruhiwa katika miripuko pacha ya mabomu iliyotokea katika mji mkuu wa Somalia Mogadishu.
Hakuna kundi lililodai kuhusika na miripuko hiyo ambayo ilitokea jana Jumamosi.
Siku ya Ijumaa pia watu wasiopungua 12 waliuawa wakati gari lililokuwa limebeba wanajeshi lilipokanyaga bomu lililotegwa ardhini katika jimbo la Kusini Magharibi.
Mnamo Agosti 3, watu wapatao 37 waliuawa katika shambulio la bunduki lililotokea kwenye ufukwe maarufu katika mji mkuu wa Somalia.
Tangu mwaka 2007, kundi la kigaidi la Al Shabab limekuwa likipambana na Serikali ya Somalia na vikosi vya kulinda amani vya Umoja wa Afrika.
Al Shabab imeongeza mashambulizi tangu Rais Hassan Sheikh Mohamud alipotangaza kuanzishwa "vita kamili vya pande zote" dhidi ya kundi hilo la kigaidi.../