Ajali za basi zaua watu 21 Kenya na Uganda
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i115432-ajali_za_basi_zaua_watu_21_kenya_na_uganda
Watu wasiopungua 21 wamepoteza maisha na makumi ya wengine kujeruhiwa katika ajali za mabasi huko Uganda na Kenya.
(last modified 2024-08-20T03:34:19+00:00 )
Aug 20, 2024 03:34 UTC
  • Ajali za basi zaua watu 21 Kenya na Uganda

Watu wasiopungua 21 wamepoteza maisha na makumi ya wengine kujeruhiwa katika ajali za mabasi huko Uganda na Kenya.

Ajali ya kwanza ilitokea Jumatatu katika eneo la Masaka kati mwa Uganda ambapo watu wanane walipoteza maisha wakati basi walimokuwa lilipoanguka kutokana na kasi ya juu. Imedokezwa kuwa dereva alijaribu kupita gari ililokuwa mbele yake lakini akashindwa kulidhibiti basi ambalo lilijipata kwenye njia ya lori lililokuwa likija likiwa limepakia unga wa mahindi.

Polisi wamethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwa sasa wanaendelea na uchunguzi. Kamanda wa Polisi mkoani Masaka Twaha Kasirye alitaja sababu ya ajali hiyo kuwa ni kasi ya juu na kubainisha kuwa dereva alikuwa akiharakisha kutimiza ratiba yake jijini Kampala.

Kulingana na ripoti ya hivi punde ya trafiki na usalama Uganda ilikumbwa na ongezeko la asilimia 30 ya vifo vya barabarani katika mwaka uliopita, ambapo vifo 4,179 vilirekodiwa. Katika kukabiliana na ongezeko la idadi ya ajali, serikali ya Uganda imeanzisha hatua mpya za usalama barabarani.

Wakati huo huo mapema leo asubuhi watu wasiopungua 13 wamepoteza maisha katika ajali mbaya ambapo basi limeanguka katika eneo la Migaa katika barabra ya Nakuru-Eldoret. Ajali hiyo iliyojiri saa 11 alfajiri ilijumuisha magari kadhaa na taarifa za awali sinasema watu 36 wamejeruhiwa. Mwaka jana jumla ya watu 4,324 walipoteza maisha katika ajali za barabarani nchini Kenya.