Bunge la Ghana lakataa kubadilsha tarehe ya uchaguzi mkuu
Bunge la Ghana limekataa kupasisha hoja ya kubadilisha tarehe ya uchaguzi mkuu nchini humo unaotazamiwa kufanyika baadaye mwaka huu.
Habari zinasema kuwa, hoja hiyo ilikosa kupata uungaji mkono wa thuluthi mbili ya wabunge ili tarehe ya uchaguzi ibadilishwe kutoka Disemba 7 kama ilivyopangwa na kurejeshwa nyuma hadi Novemba 7. Tume ya Uchaguzi ya Ghana iliwasilisha hoja hiyo bungeni kwa hoja kuwa, tarehe ya uchaguzi huo inafaa kurejeshwa nyuma ili kutoa fursa ya uchaguzi huo kuingia duru ya pili iwapo mshindi hatapatikana katika duru ya kwanza.
Vyama vya upinzani nchini humo vimepiga hoja hiyo vikidai kuwa, kurejeshwa nyuma tarehe ya uchaguzi kutaikosesha Tume ya Uchaguzi wakati wa kutosha wa kuuandaa uchaguzi wenyewe.
Mapema mwezi Aprili, maelfu ya wananchi wa Ghana wakiongozwa na vyama vya upinzani walifanya maandamano katika miji kadhaa ya nchi hiyo wakitaka kufanyiwa marekebisho sheria za uchaguzi nchini humo.
Baadaye mwezi huo, Tume ya Uchaguzi ya Ghana ilitangaza kuwa imekubaliana na ombi la kuzifanyia marekebisho sheria za uchaguzi, kwa lengo la kuongeza uwazi katika mchakato wa uchaguzi.