Watu 21 wauawa katika hujuma ya waasi wa ADF nchini DRC
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i136446-watu_21_wauawa_katika_hujuma_ya_waasi_wa_adf_nchini_drc
Takriban watu 21 wameuawa katika shambulio la hivi karibuni linalohusishwa na waasi wa Allied Democratic Forces (ADF) mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), afisa mmoja amesema Jumatatu.
(last modified 2026-02-10T02:25:38+00:00 )
Feb 10, 2026 02:25 UTC
  • Watu 21 wauawa katika hujuma ya waasi wa ADF nchini DRC

Takriban watu 21 wameuawa katika shambulio la hivi karibuni linalohusishwa na waasi wa Allied Democratic Forces (ADF) mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), afisa mmoja amesema Jumatatu.

Shambulio hilo lilitokea Ijumaa katika eneo la Lubero, likilenga makazi ya kikundi cha Bapakombe katika jimbo la Kivu Kaskazini.

Boniface Kanyamulamba, mkuu wa kikundi cha Bapakombe, amezungumza na waandishi wa habari mjini Lubero na kusema: “Idadi ya vifo kutokana na shambulio la ADF imeongezeka hadi 21 kutoka 14 zilizoripotiwa awali, baada ya miili zaidi kupatikana Jumapili,” amesema

“Aidha, vijiji vitatu—Boti, Isigo na Mambimbi—vililengwa katika mashambulio haya ya wakati mmoja. Waasi hao pia walichoma nyumba nyingi, huku watu kadhaa wakibaki hawajulikani walipo kufuatia mashambulio hayo.”

Wimbi la hivi karibuni la mashambulizi ya waasi katika eneo hilo limesababisha uhamiaji mkubwa wa wakazi, ambapo wananchi wamekimbilia maeneo yanayochukuliwa kuwa salama zaidi katika mji wa Kambau, kwa mujibu wa taarifa za vyombo vya habari vya ndani.

Kutokana na hali hiyo, mazingira ya usalama yamelemaza shughuli za kila siku, yakikatiza elimu, biashara, na shughuli nyingine za kijamii na kiuchumi katika maeneo kadhaa.

Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, mwaka 2025 Kongo ilikumbwa na mgogoro wa kibinadamu usio na kifani, uliosababishwa na migogoro ya silaha inayoendelea, uhamiaji wa watu kwa wingi, misukosuko ya hali ya hewa, pamoja na milipuko ya mara kwa mara ya magonjwa.

Mashariki mwa Kongo inaendelea kuwa miongoni mwa maeneo yenye hali tete zaidi kiusalama, huku zaidi ya raia 60 wakiripotiwa kuuawa tangu mwanzoni mwa 2026 katika maeneo ya Beni na Lubero, kwa mujibu wa mashirika ya kiraia.

Tangu mwaka 2021, majeshi ya Uganda na Kongo yamekuwa yakitekeleza operesheni za pamoja za kijeshi dhidi ya ADF.

Kundi hilo, ambalo limekuwa likifanya shughuli zake mashariki mwa Kongo kwa miaka kadhaa, lilitangaza utii wake kwa ISIS (Daesh) mwaka 2019.