OCHA: Takribani raia 50 wameuawa katika mapigano mashariki mwa DRC
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i136794-ocha_takribani_raia_50_wameuawa_katika_mapigano_mashariki_mwa_drc
Takribani raia 50 wameuawa wakati wa mapigano yaliyozuka mwezi Januari kati ya vikosi vinavyoiunga mkono serikali na waasi wenye silaha katika jimbo la Kivu Kaskazini, mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC). Hayo ni kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa Jumatano na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Masuala ya Kibinadamu (OCHA).
(last modified 2026-02-19T07:42:35+00:00 )
Feb 19, 2026 07:42 UTC
  • OCHA: Takribani raia 50 wameuawa katika mapigano mashariki mwa DRC

Takribani raia 50 wameuawa wakati wa mapigano yaliyozuka mwezi Januari kati ya vikosi vinavyoiunga mkono serikali na waasi wenye silaha katika jimbo la Kivu Kaskazini, mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC). Hayo ni kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa Jumatano na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Masuala ya Kibinadamu (OCHA).

Kwa mujibu wa ripoti hiyo ya hali, mapigano yalitokea kati ya Januari 12 na 16 katika zaidi ya vijiji kumi na viwili ndani ya eneo la Rutshuru, yakiathiri hasa makundi ya Bukombo, Kihondo, Mutanda, Bambo na Tongo.

OCHA imeeleza kuwa watu kadhaa walijeruhiwa, huku wengine wengi wakilazimika kuyahama makazi yao na kukimbilia maeneo salama zaidi katika eneo la Masisi. Mapigano hayo yaliwakutanisha waasi wa muungano wa AFC/M23 dhidi ya wanamgambo wanaoiunga mkono serikali wanaojulikana kama Wazalendo.

Katika tukio jingine tofauti, watu 11 waliuawa na takribani 40 kujeruhiwa kufuatia shambulizi la anga la jeshi dhidi ya ngome za waasi mapema mwezi Januari katika kituo cha Masisi, ripoti hiyo iliongeza.

Muungano wa waasi wa Alliance Fleuve Congo (AFC/M23), unaohusisha kundi la waasi la M23, umekuwa kiini cha mgogoro unaoendelea mashariki mwa Congo.

Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, kundi hilo la waasi linaungwa mkono na nchi jirani ya Rwanda, madai ambayo Kigali imekuwa ikiyakanusha mara kwa mara. Hata hivyo, AFC/M23 inadhibiti maeneo makubwa mashariki mwa Congo, yakiwemo miji mikuu ya majimbo ya Goma na Bukavu, iliyotekwa mapema mwaka 2025.

Wiki iliyopita, ofisi ya rais wa Congo ilitangaza kukubali mapendekezo ya Angola ya kusitisha mapigano kati ya serikali na AFC/M23 kuanzia Februari 18. Hata hivyo, hadi Jumatano, haikuwa wazi iwapo pande zote mbili zilikuwa zikiheshimu makubaliano hayo ya usitishaji mapigano.