Wamorocco wataka uadilifu dhidi ya wauaji wa muuza samaki
Kwa mara nyingine maelfu ya raia wa Morocco wamefanya maandamano makubwa katika mji wa Al Hoceima kaskazini magharibi mwa nchi hiyo wakitaka kutekelezwa uadilifu katika faili la mauaji ya Mouchine Fikr, muuza samaki aliyeuawa mwishoni mwa mwezi Oktoba mwaka huu.
Waandamanaji wametoa nara dhidi ya serikali ya nchi hiyo sambamba na kutaka kutekelezwa uadilifu kwa wahusika wa kifo cha muuza samaki huyo ambacho kiliibua wimbi la malalamiko ya nchi nzima. Baadhi ya waandamanaji walibeba bendera zilizokuwa na picha za watu wa kabila la walio wachache la Amazigh na picha ya Abdul-Karim al-Khatabi, mkuu wa kile kinachoitwa Jamhuri ya Reef, ambayo ilitangaza uhuru wake wa muda mfupi hapo mwaka 1920 wakati wa mapinduzi dhidi ya wavamizi wa Uhispania.
Mouchine Fikr ni kijana aliyekuwa na umri wa miaka 30, aliuawa kwa kufinywafinywa na mashine ya gari la kuzoa taka wakati akijaribu kuchukua samaki wake aliokuwa akiwauza ambao walichukuliwa na polisi na kutupwa katika gari hilo tarehe 28 Oktoba mwaka huu mjini Al Hoceima. Mouhcine Fikri alikuwa amenunua sakamaki wake hao bandarini kabla ya kupokonywa na polisi kufuatia marufuku ya wakuu wa eneo hilo ya kuuza baadhi ya samaki.
Mwanzoni mwa mwezi huu, Waziri Mkuu wa Morocco, Abdelilah Benkirane alitangaza kuwa, serikali ya Rabat itawachukulia hatua kali wahusika wa mauaji ya Fikri, katika hali ambayo hadi sasa hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa dhidi yao.