Wapinzani wapigwa marufuku kufanya maandamano Congo DR
Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imepiga marufuku maandamano ya kambi ya upinzani.
Polisi ya Congo imetangaza kuwa, maandamano yaliyoitishwa na wapinzani wa serikali kote nchini hayataruhusiwa. Tangazo hilo limetolewa baada ya kambi ya upinzani kuitisha maandamano ya nchi nzima baada ya Rais Joseph Kabila kumteua Waziri Mkuu mpya ambaye haridhiwi na kambi ya upinzani.
Maandamano hayo yalipangwa kufanyika Jumatatu ya leo mjini Kinshasa na miji mingine ya nchi hiyo. Hata hivyo jeshi la polisi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo limetangaza kuwa litatawanya mkusanyiko wowote wenye zaidi ya watu 10.
Chama kikuu cha upinzani cha UDPS katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kimevitaka vyama vyote vya upinzani kushiriki katika maandamano ya leo.
Mgogoro wa kisiasa katika Congo DR ulianza baada ya Rais Joseph Kabila wa nchi hiyo kukataa kuondoka madarakani licha ya kipindi chake cha muhula wa pil kumalizika. Ripoti zinasema tangu mwezi Septemba mwaka jana hadi sasa watu 400 wameuawa nchini humo katika ghasia na machafuko yanayoendelea kwenye miji mbalimbal;i ya nchi hiyo.