UN: Kuna haja ya kufanyika mazungumzo ili kumaliza mapigano Kongo DR
Mshauri wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya kuzuia mauaji ya umati, amezitaka pande za mapigano huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kufanya mazungumzo ili kukomesha vitendo vya utumiaji mabavu nchini humo.
Adama Dieng ameyasema hayo huko Kinshasa, mji mkuu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ambapo sambamba na kusisitizia wajibu wa kufanyika mazungumzo ya kumaliza mapigano na machafuko nchini humo, amesema kuwa serikali ndiye muhusika mkuu katika kuimarisha usalama na amani, kusimamia utawala wa sheria na kuzuia utumiaji nguvu na mabavu.
Kadhalika Adama Dieng akimalizia kazi yake iliyodumu yapata wiki moja katika kufuatilia hali ya usalama nchini humo amelaani vikali vitendo vya ukatili vinavyofanyika katika baadhi ya mikoa ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Mshauri wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya kuzuia mauaji ya umati aliwasili mjini Kinshasa tarehe 19 ya mwezi huu ambapo alikutana na makundi tofauti ya kijamii na kufanya nayo mazungumzo ya kuitafutia ufumbuzi mizozo mbalimbali na kisiasa na kukomesha mapigano yanayoendelea katika maeneo kadhaa ya nchi hiyo ya katikati mwa Afrika.
Maeneo ya mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo yamekuwa yakishuhudia machafuko kwa zaidi ya miaka 20 sasa ambapo maelfu ya watu wameshauawa na wengine wengi kuwa wakimbizi.