Jeshi la Somalia na kikosi cha AU chakomboa mji wa Janale
Wanajeshi wa serikali ya Somalia na wale wa kulinda amani wa Umoja wa Afrika wameukomboa mji Janale ulioko kusini mwa nchi hiyo ambao ulikuwa ukishikiliwa na wanamgambo wa kundi la al Shabab.
Maafisa wa serikali ya Somalia wametangaza kuwa, wanajeshi wa nchi hiyo na kikosi cha kudumisha amani cha Umoja wa Afrika jana waliukomboa mji wa Janale uliokuwa ukishikiliwa na kundi la al Shabab kufuatia mapigano makali yaliyojiri baina ya pande hizi katika eneo la Shabele ya Chini kusini mwa Somalia.
Kanali Hassan Mohamed Abukar wa jeshi wa Somalia amesema kuwa, kikosi cha pamoja cha jeshi la Somalia na Umoja wa Afrika kimetekeleza vizuri oparesheni dhidi ya al Shabab na kufanikiwa kuyakomboa maeneo kadhaa ukiwemo mji wa Janale.
Ameongeza kuwa, wanajeshi wa Somalia na wale wa AU wataendelea na oparesheni zao za kijeshi ili kulikomboa kikamilifu eneo zima la Shabele ya Chini.
Hii ni katika hali ambayo kundi la kigaidi la al Shabab pia limethibitisha kujiri mapigano hayo na kudai kuwa, limeuwa wanajeshi kadhaa wa kikosi cha AU na wa jeshi la Somalia. Hata hivyo maafisa wa jeshi wa Somalia wamekadhibisha madai hayo ya al Shabab.