UN yatahadharisha kuhusu mgogoro wa Congo DR
Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya misaada ya kibinadamu ametahadharisha kuhusu mgogoro mkubwa unaisumbua Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Stephen O’Brien amesema baada ya kutembelea mikoa ya mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kwamba, mgogoro wa kibinadamu nchini humo umefikia kiwango cha hatari.
O’Brien amesema kumeanzishwa kambi nyingi za muda katika maeneo yenye machafuko huko mashariki mwa Congo DR na kusisitiza kuwa: Raia wengi wa maeneo hayo wamekimbia makazi na nyumba zao kwa shabaha ya kuokoa maisha yao kutokana na mashambulizi na mapigano ya kikabila.
Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amesema kuwa, watu wasiopungua laki tano wamelazimika kuwa wakimbizi katika mkoa wa Tanganyika pekee kutokana na machafuko na mapigano ya ndani.
Wakati huo huo Jumuiya ya Madaktari Wasio na Mipaka imetangaza kuwa, ina wasiwasi mkubwa kuhusu ukosefu wa suhula na chakula cha kutosha kwa ajili ya kukabiliana na mgogoro mkubwa wa wakimbizi katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.