Maiti 8 za wahajiri zapatikana katika boti ya plastiki Libya
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i32596-maiti_8_za_wahajiri_zapatikana_katika_boti_ya_plastiki_libya
Miili 8 ya wahajiri waliokuwa wakielekea barani Ulaya imepatikana ndani ya boti ya plastiki na wapiga mbizi wa shirika moja lisilo la serikali katika pwani ya Libya.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Aug 02, 2017 03:46 UTC
  • Maiti 8 za wahajiri zapatikana katika boti ya plastiki Libya

Miili 8 ya wahajiri waliokuwa wakielekea barani Ulaya imepatikana ndani ya boti ya plastiki na wapiga mbizi wa shirika moja lisilo la serikali katika pwani ya Libya.

Shirika hilo la wapiga mbizi la Uhispania la Proactiva Open Arms limesema maiti hizo ziligunduliwa na meli ya wafanya biashara ya Santa Lucia na kisha kuokolewa na maafisa wa Gadi ya Pwani ya Libya. 

Habari zinasema, miili ya wanawake ni miongoni mwa maiti hizo zilizopatikana karibu na pwani ya Libya jana Jumanne.

Wiki ilioyopita, Gadi ya Pwani ya Libya ilitangaza habari ya kuokolewa wahajiri haramu 300 karibu na miji ya Zawiya na Sabratha katika maji ya pwani ya magharibi mwa mji mkuu Tripol. Aidha miili 13 za wahajiri wengine waliokufa maji ilipatikana.

Wahajiri wa Kiafrika katika boti ya plastiki wakielekea Ulaya

Tangu mwanzoni mwa mwaka huu, karibu wahajiri elfu mbili wamepoteza maisha yao ndani ya bahari ya Mediterrania, wakiwa katika safari hatari za kuelekea Ulaya kutafuta ajira na maisha bora.

Kwa mujibu wa Shirika la Wahajiri Duniani (IOM), wahajiri zaidi ya elfu tano aghlabau wakiwa raia wa nchi za Nigeria, Eritrea, Somalia, Sudan, Gambia, Senegal, Mali, Morocco na Tunisia walifariki dunia kwa kuzama katika bahari ya Mediterrania wakiwa katika safari hizo hatari za kuelekea Ulaya.