9 wauawa katika makabiliano baina ya vikosi tofauti vya usalama Somalia
Kwa akali watu tisa wameuawa katika makabiliano baina ya wanajeshi na maafisa wa polisi katika mji mkuu wa Somalia, Mogadishu.
Meja Abdullahi Hussein, afisa wa ngazi za juu wa polisi mjini hapo ameliambia shirika la habari la Reuters kuwa, mapigano hayo ya jana Jumamosi yalianza baada ya maafisa wa polisi kuwashambulia askari wa Jeshi la Taifa la Somalia wakidhani kuwa ni wanamgambo wa magenge ya kigaidi.
Amesema kabla ya kuanza makabiliano hayo, polisi ya Somalia ilikuwa imepatiwa taarifa za kiintelijensia kwamba kuna wanachama wa makundi ya kigaidi katika eneo palipotokeo mapigano hayo ya jana mjini Mogadishu.
Haya yanajiri siku chache baada ya kundi la kigaidi na kitakfiri la al-Shabaab kuua askari 24 wa Somalia kwa kulipua gari lililokuwa limetegwa mabomu katika eneo la Bulla Hawa.
Mashambulizi ya kigaidi ya kundi la al-Shabaab yanayoendelea kwa kipindi cha zaidi ya miaka kumi sasa nchini Somalia yameua maelfu ya watu na kuwalazimisha mamilioni ya wengine kuwa wakimbizi.