Marekani imezidisha harakati zake za kijeshi nchini Somalia
Kamandi ya jeshi la Marekani barani Afrika imetangaza kuwa nchi hiyo imeongeza kiwango cha harakati zake za kijeshi nchini Somalia.
Kamandi ya jeshi la Marekani barani Afrika imedai kuwa katika saa 24 zilizopita jeshi la nchi hiyo limefanya mashambulio matatu ya anga dhidi ya wanamgambo wenye misimamo ya kufurutu mpaka ndani ya ardhi ya Somalia.
Msemaji wa kamandi hiyo alitangaza jana kuwa mashambulio ya ndege za Marekani zisizo na rubani za droni nchini Somalia yamesababisha kuuliwa wanamgambo kadhaa wabeba silaha wenye misimamo ya kufurutu mpaka.
Kitambo fulani nyuma Marekani ilitangaza kuwa imezishambulia ngome kadhaa za makundi ya kigaidi nchini Somalia.
Ijapokuwa kundi la kigaidi na ukufurishaji la Daesh (ISIS) limepanua harakati zake katika eneo la Pembe ya Afrika huku kundi la kigaidi la Al-Shabaab lenye mfungamano na mtandao wa Al-Qaeda nalo pia likiwa linaendeleza mashambulio nchini Somalia kwa miaka kadhaa sasa, lakini radiamali ya kuchelewa ya Marekani kuhusiana na makundi hayo inadhihirisha mbinu na hila mpya inayofanywa na Washington kwa lengo la kupanua wigo wa kuwepo kwake kijeshi katika eneo hilo.
Kwa mujibu wa taarifa za kiintelijinsia kutoka Afghanistan, Iraq na Syria, Marekani, ambayo yenyewe imehusika katika uundaji wa makundi ya kigaidi na yenye misimamo ya kufurutu mpaka kama Daesh, Al-Qaeda na Taliban, baada ya kupita muda tangu kuyaasisi makundi hayo imeandaa mazingira ya kujiingiza kijeshi kwenye nchi yalikojizatiti kwa kisingizio cha kupambana nayo.
Kuwepo kijeshi Washington nchini Afghanistan, kabla yake huko Iraq na hatimaye kuunda muungano eti wa kupambhana na Daesh nchini Syria, yote hayo yanatathminiwa katika muelekeo huo.../