Tanzania kupoteza wawekezaji baada ya kujitoa kwenye taasisi za kimataifa za usuluhishi
Wataalamu wanasema kuwa, uamuzi uliochukuliwa na serikali ya Tanzania wa kurekebisha sheria ya Ushirikiano wa Sekta ya Umma na Binafsi PPP na kujitoa kwenye taasisi za kimataifa za usuluhishi utawatia hofu wawekezaji, na kupelekea uhusiano wa nchi hiyo na mashirika ya fedha duniani kuwa mgumu zaidi.
Mhadhiri wa masomo ya uchumi wa Chuo Kikuu cha Mzumbe nchini Tanzania Bw. Honest Ngowi ametoa tahadhari hiyo katika mahojiano aliyofanyiwa na shirika la habari la Xinhua na kusema kuwa, uamuzi wa kujitoa kwenye vyombo vya kimataifa vya usuluhishi utafukuza wawekezaji, kwani wengi wao wanapendelea vyombo hivyo kutatua mikwaruzano.
Naye Mbunge wa Kigoma Mjini Bw. Zitto Zuberi Kabwe amesema, uamuzi huo utarudisha nyuma juhudi za kuvutia wawekezaji wengi zaidi kwa ajili ya kuendeleza uchumi wa viwanda.

Kabwe amesema, Tanzania ni mwanachama wa Benki ya Dunia ambayo moja ya taasis zake tanzu ni Kituo cha Kimataifa cha Usuluhishi wa Migogoro ya Uwekezaji (ICSID) hivyo hatua ya Tanzania ya kujiondoa katika ICSID ni sawa na kujiondoa katika Benki ya Dunia.
Siku ya Jumatano Tanzania ilirekebisha sheria ya Ushirikiano wa Sekta ya Umma na Binafsi PPP, na kuzipa mahakama za nchi hiyo madaraka ya kutatua mikwaruzano ya uwekezaji badala ya vyombo vya kimataifa vya usuluhishi. Tanzania imedai kuwa vyombo vya kimataifa vya usuluhishi vina ubaguzi, hivyo imeiwajibisha serikali ya nchi hiyo kutumia mahakama za ndani.