Ghasia zaibuka Ethiopia kufuatia kuongezeka mapigano ya kikabila
Ghasia zimeshika kasi nchini Ethiopia kufuatia kuongezeka mapigano ya kikabila katika eneo la kaskazini mashariki mwa nchi hiyo.
Waandamanaji katika mkoa wa Afar, kaskazini mashariki mwa nchi hiyo jana walifunga njia kuu inayoelekea upande wa bahari. Kwa mujibu wa habari hiyo, ghasia hizo ziliibuka Jumapili iliyopita sambamba na kufunga njia kuu inayoziunganisha Ethiopia na Djibouti. Waandamanaji wanaikosoa serikali kuu ya Addis Ababa ya kuwapeleka askari jeshi eneo hilo badala ya wanamgambo wa kieneo ambao wamekuwa wakiwalinda raia. Kufuatia hali hiyo waandamanaji wametangaza kwamba wataendelea na maandamano hayo hadi pale serikali itakapobadili uamuzi wake huo.
Wakosoaji wa Abiy Ahmed, Waziri Mkuu wa nchi hiyo wanaamini kwamba marekebisho ya kisiasa aliyoyafanya ndiyo yameibua tena mapigano ya kikabila nchini humo. Mapigano ya kikabila ya mwaka jana nchini Ethiopia yalipelekea karibu watu milioni tatu kuwa wakimbizi. Mapigano ya mwisho ya kikabila ni yale yaliyoshuhudiwa kati ya watu wa kabila la Afars na Issa Somalia ambazo ni jamii za wachache katika eneo hilo na ambayo yalitokea mwezi Disemba uliopita. Katika mapigano hayo makumi ya watu waliuawa.