Foreign Policy: Waziri Mkuu wa Ethiopia ni mwanafikra wa kimataifa
Jarida la Foreign Policy limemtaja Abiy Ahmed, Waziri Mkuu wa Ethiopia kuwa mwanafikra wa kimataifa kutokana na jitihada zake za kitaifa na kieneo ndani ya miezi 12 iliyopita.
Jarida hilo limesema ndani ya miezi tisa katika uongozi wake, Abiy amefanya mabadiliko mengi katika nyuga za uchumi, siasa na diplomasia mbali na kuhuisha uhusiano na majirani zake.
Serikali ya Abiy Ahmed imewaachia huru maelfu ya wafungwa wa kisiasa katika fremu ya marekebisho ya haraka ya kisiasa na kiuchumi ambayo yanashuhudiwa katika nchi hiyo ya Pembe ya Afrika tokea Waziri Mkuu, Abiy Ahmed aingie madarakani mwezi Aprili mwaka jana.
Mbali na jitihada zake ndani ya nchi, Abiy pia amekuwa mbioni kufufua uhusiano wa nchi hiyo na nchi za kieneo. Julai 9 mwaka jana, Waziri Mkuu huyo wa Ethiopia, na Rais wa Eritrea, Isaias Afwerki walisaini makubaliano ya kukomesha uhasama na kuhuisha uhusiano wao wa kidiplomasia katika hafla iliyofanyika mjini Asmara.