Watu 21 wauawa katika mapigano yanayoendelea nchini Libya
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i52700-watu_21_wauawa_katika_mapigano_yanayoendelea_nchini_libya
Wizara ya Afya ya Serikali ya Maafikiano ya Kitaifa ya Libya imetangaza kuwa, watu wasiopungua 21 wameuawa na wengine 27 kujeruhiwa kufuatia mapigano makali yanayoendelea kando kando ya mji mkuu Tripoli.
(last modified 2026-02-05T09:20:29+00:00 )
Apr 08, 2019 00:01 UTC
  • Watu 21 wauawa katika mapigano yanayoendelea nchini Libya

Wizara ya Afya ya Serikali ya Maafikiano ya Kitaifa ya Libya imetangaza kuwa, watu wasiopungua 21 wameuawa na wengine 27 kujeruhiwa kufuatia mapigano makali yanayoendelea kando kando ya mji mkuu Tripoli.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa, mapigano kati ya vikosi vya Serikali ya Maafikiano ya Kitaifa na vile vinavyoongozwa na Jenerali Khalifa Haftar yamesababisha kwa uchache watu 21 kuuawa huku mapigano hayo yakiripotiwa kuendelea.

Jenerali Khalifa Haftar ambaye vikosi vyake vinasonga mbele kuelekea mji mkuu Tripoli ametoa ujumbe wa sauti akiwataka wananchi wa Tripoli kutokabiliana na vikosi vyake.

Mapigano hayo  ambayo yamezusha wasiwasi mkubwa miongoni mwa raia wa Tripoli yamehatarisha juhudi za kieneo na kimataifa za kuupatia ufumbuzi mgogoro wa Libya kupitia njia ya mazungumzo na utatuzi wa kisiasa.

Jenerali Khalifa Haftar

Hayo yanajiri katika hali ambayo, mkutano wa kitaifa wa Libya umepangwa kufanyika Julai mwaka huu huko Addis Ababa mji mkuu wa Ethiopia chini ya usimamizi wa Umoja wa Mataifa. 

Utata huo mkubwa umejitokeza hivi sasa huko Libya katika hali ambayo wiki iliyopita, taasisi nne za kimataifa yaani Umoja wa Mataifa, Umoja wa Afrika, Umoja wa Ulaya na Jumuiya ya Nchi za Kiarabu zilielezea matumaini yao kwamba mkutano wa makundi yote ya Libya uliopangwa kufanyika mwezi Julai utaleta utulivu nchini humo na kusaidia kuundwa serikali na taasisi zake zenye nguvu.